Home Tetesi za usajili YANGA, SIMBA ZAWANIA SAINI YA BEKI HUYU WA KUSHOTO

YANGA, SIMBA ZAWANIA SAINI YA BEKI HUYU WA KUSHOTO


 BAADA ya Simba kuwa katika mipango ya kukamilisha usajili wa beki wa kushoto wa timu ya taifa ya Tanzania, Nickson Kibabage, hatimaye Klabu ya Yanga nayo imeingilia kati dili hilo kwa ajili ya kutaka kumsajili beki huyo ambaye ameonekana kuwa tishio.

 

Hivi karibuni uongozi wa Simba ulikutana na mchezaji huyo kwa mazungumzo ya kutaka kumsajili alipokuwa nchini katika kambi ya timu ya taifa ya Tanzania, lakini kwa sasa inaripotiwa Yanga pia imeingilia kati dili hilo ikijaribu kumshawishi ili akubali kujiunga na timu hiyo.

 

Kibabage kwa sasa anakipiga katika Klabu ya Youssoufia FC ya nchini Morroco, akitokea kwa mkopo katika Klabu ya Difaa Hassan El Jadid ya nchini humo.

 

Chanzo cha uhakika kutoka Yanga kimeeleza kuwa timu hiyo ipo katika mipango ya kuboresha kikosi chao kwa ajili ya msimu ujao haswa katika eneo la beki wa kushoto jambo ambalo limewafanya kuanza kuingia sokoni mapema huku Kibabage akiwa mmoja kati ya mapendekezo yao.

 

“Ni kweli Yanga tupo katika mpango wa kuendelea kukisuka kikosi chetu kwa ajili ya mipango yetu ya baadaye na moja kati ya sehemu ambazo zinatakiwa kufanyia maboresho ni pamoja na eneo letu la ulinzi wa kushoto.

 

“Ndiyo maana umeona kuna tetesi nyingi zinatuhusisha na wachezaji wa maeneo hayo, kuhusiana na Kibabage ni moja kati ya wachezaji wazuri katika eneo la ulinzi wa kushoto, ni mchezaji ambaye tumekuwa tukimfikiria kuwa moja kati ya sehemu ya wachezaji wetu,tutaona itakuwaje mwisho wa msimu huu,” kilisema chanzo.

 

Alipotafutwa beki Nickson Kibabage juu ya kuhitajika ndani ya Yanga aligoma kabisa kusema chochote juu ya taarifa hizo.

Chanzo:Championi

SOMA NA HII  FARID MUSSA 'ASUKUMIWA' SIMBA....MABOSI YANGA WAMPA UKWELI KUWA HATAKIWI....