Home Makala ISHU YA LAMINE, MNATA NA SAIDO BADO NI TATIZO KWA YANGA

ISHU YA LAMINE, MNATA NA SAIDO BADO NI TATIZO KWA YANGA


BADO kuna jambo la kufanya kwenye kikosi cha Yanga hasa katika suala la nidhamu ambayo inaonekana kuna mahali hapapo sawa.

Imekuwa kawaida kwa hivi karibuni kuwaona wachezaji wa Yanga wakizinguana wenyewe kwa wenyewe na muda mwingine na mashabiki wao jambo ambalo halina afya kwa maendeleo ya soka.

Ipo wazi kwamba kwa sasa kuna wachezaji wawili ambao wamewekwa kando na Yanga kutokana na ishu ya utovu wa nidhamu hivyo ni muhimu kuangalia wapi wanakwama.

Wakati wanajiandaa na mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Biashara United wapo wachezaji ambao wamewekwa kando kutokana na ishu ya nidhamu.

Zipo timu nyingine ambazo zinafanya mambo hayo ila inakuwa ni nje ya uwanja na haionekani hadharani kama inavyotokea kwa Yanga.

Ikumbuke ishu ya Saido Ntibanzokiza namna alivyozinguana na wachezaji wenzake pamoja na kocha wa zama zile Juma Mwambusi ikiwa ni suala la kucheza na kufunga bao jambo ambalo alikasirika sababu ya kuanzia benchi.

Bado alibebwa na kuzungumza kwamba ilikuwa ni sehemu ya mchezo basi ikiwa kutakuwa na mwendelezo huu kuna mahali hapapo sawa. 

Lamine Moro nyota wa Yanga ambaye ni nahodha pia amewekwa kando kwa muda kutokana na kile ambacho kimeelezwa kuwa ni utovu wa nidhamu.

Nyota huyo amekuwa kwenye mvutano mkubwa na mabosi wake ambapo mara ya mwisho aliondolewa kwenye kambi ya timu hiyo ilipokuwa na mchezo wa ligi dhidi ya Namungo FC.

Baada ya hapo hajaonekana kwenye kikosi cha Yanga na hakuwa kwenye msafara wa kikosi kilichokwea pipa kuibukia Tabora kwa ajili ya mchezo wa Kombe la Shirikisho dhidi ya Biashara United.

Mbali na Lamine pia kipa wao namba moja, Metacha Mnata naye pia hatakuwa sehemu ya kikosi kutokana na tatizo la utovu wa nidhamu.

Mnata alisimamishwa hivi karibuni baada ya kuonyesha ishara isiyo na tafsri nzuri kwa mashabiki jambo ambalo limefanya nyota huyo asimamishwe.

Basi kwa kuwa Yanga ni timu kongwe inapaswa kuwa mfano kwa Mwadui FC, Gwambina, Njombe Mji pamoja na Kagera Sugar ambao hawajawa na matukio ya namna hii.


Itazame namna Polisi Tanzania inavyoshughulikia masuala ya nidhamu, ilisimamisha wachezaji wake wote ambao  walikuwa na mwendo mbovu na wale ambao waliweza kujirekebisha walirudi kikosini.

SOMA NA HII  EXCLUSIVE...GYAN AFUNGUKA ALIVYOLAZIMISHWA KUFANYA ASIYOYAPENDA NA KIBOSILE WA SIMBA...

Iwe hivyo kwa kila timu mafanikio yanabebwa na nidhamu.