Home news UCHAGUZI MKUU TFF..CHONDECHONDE, WABUNGE MSITUINGIZE MATATIZONI

UCHAGUZI MKUU TFF..CHONDECHONDE, WABUNGE MSITUINGIZE MATATIZONI

 


MACHO ya wapenda mpira sasa yamehamia 
katika uchaguzi Mkuu wa Shirikisho la Soka Tanzania (TFF). Sasa ni nani atachukua, nani atarudisha na nani atashinda.

Pamoja na hivyo, gumzo limezidi si kwa uchaguzi tu bali yale malalamiko ya baadhi ya wabunge wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kuhusiana na suala la ugombea wa nafasi ya urais.

Mbunge wa Mwera, Zahoro Mohammed amelalamika kwamba ameshindwa kupata vigezo vya kugombea kwa madai kwamba kumekuwa hakuna haki ndani ya Shirikisho la Soka Tanzania (TFF).

Sheria ya uchaguzi wa shirikisho hilo una kanuni ya kila mgombea kupata kura tano kutoka kwa wanachama wa TFF ambao wako zaidi ya 40. Mbunge Mwera anasema kila anapokwenda kuchukua hizo (endorsement) anajikuta zimeshachukuliwa. Hivyo anaona kama anaonewa na ndio maana analalamika.

Ukifuatilia malalamiko yao, ni kwamba anaona kwamba ameonewa na anaona Rais wa sasa wa TFF, Wallace Karia amechukua endorsement nyingi na anaona alizichukua kabla ya shughuli nzima ya uchukuaji wa fomu.

Tayari Mwenyekiti wa kamati ya uchaguzi, Kiomon Kibamba tayari ameelezea kuwepo kwa kanuni na sheria za uchaguzi. Hivyo ni lazima wafuate taratibu hizo.

Malalamiko kwamba wana hofu kuwa Karia atakuwa alichukua mapema udhamini huo kwa maana ya endorsement. Kwamba Zahoro Mohammed alichukua fomu saa 4 asubuhi akakosa na Karia alichukua saa 8 mchana lakini akapata karibu kila mkoa ukimpitisha kuwa mgombea.

Ukiangalia kigezo hiki unaweza kujiuliza hivi ni kweli uchaguzi wa TFF uvurugwe au uvurugike kwa kigezo hiki kwa kuwa tu Mbunge wa Mwera ameshindwa kupata endorsement?

Unajiuliza hivi ni kweli inawezekana kwamba wakati anakwenda kuchukua fomu, hakuwa hata amefanya mawasiliano na wanachama?

Kama ni hivyo inaonyesha Mbunge Zahoro naye alifanya uzembe mkubwa na inaonyesha hakuwa na maandalizi ya kutosha kwa ajili ya kushiriki uchaguzi huo.

Uchaguzi ni maandalizi na sehemu ilikuwa ni lazima awe na maandalizi ya mapema badala ya hiki ambacho yeye amekifanya. Vizuri akajipange tena na ikiwezekana kama watarejea tena kwenye uchaguzi mwingine awe anajua maandalizi sahihi ni yapi na yanatakiwa kufanyika vipi.

SOMA NA HII  UZEMBE WA MABEKI SIMBA WAMTIA KIWEWE ROBERTINHO....AANZA KAZI NA CHE MALONE...

Kwa wakati huu si sahihi kuanza kulalamika kama wameonewa wakati hawakuwa wamejiandaa na hofu yangu kubwa, wabunge ambao wamejitokeza na kuwatetea wabunge wenzao, ninaamini wanaelewa maana ya uchaguzi na maandalizi yake.

Walipaswa kujiandaa, walipaswa kujipanga na kama kuna upungufu wangeujua mapema. Kushindwa kwao kuwa na maandalizi mengi wasije wakaukwamisha uchaguzi wa mpira na lengo wao kutaka kuingia kwenye madaraka.

Kwa sasa ambao walipaswa kuhojiwa hasa ni wanachama ambao wametoa endorsement kwa Karia. Wao ndio wahojiwe na si kumlalamikia Karia ambaye amepewa na si amelazimisha.

Karia yeye amepewa, au yeye ni mpokeaji. Kwa kuwa ili watoe endorsement wanakutana kamati nzima ya mkoa ambao ni mwanachama na kujadili wampe nani, baada ya hapo wanatoa kwa mtu wanayeona anafaa.

Sasa wa kuhojiwa ni Karia au watu waliompa? Jibu liko wazi na wakati huohuo ni kujifunza kwamba ili upewe au ukubalike au uaminiwe na hao wanachama hadi wakubali kutoa endorsement unatakiwa kuwa na nini?

Kazi ya Karia na timu yake imeonekana, wengine wanaogombea wanaweza kuaminika vipi? Wana mambo mangapi yanaweza kuwafanya waaminike? 

Wana hivyo vigezo na wanaweza kuwa na huo mvuto kwa wale wanachama? Mwisho pia wahusika wajiulize, kanuni hizo zilikuwepo lakini jiulize, hawa wanaozilalamikia sasa hawakuwahi kuzijua au kuzifuatilia na kwanini hatukuwahi kuwasikia wakilalamika?

Waliopitisha ni TFF na kamati zake na hawa waliotaka kugombea sasa, vipi hawakuwahi kusema kabla waseme leo wakati wa uchaguzi huku wakilia utafikiri wameonewa sana.

Chondechonge wabunge na wagombe wengine, kama mtakosa vigezo, msivuruge uchaguzi kwa hamu zemu za kutaka kuwa viongozi. Badala yake muangalie namna ambayo ni sahihi kwenu kufanya kwa ajili ya wakati mwingine.

Mnaowalalamikia ni kamati za mikoa au vyama, jiulizeni pia hawa wote hawaelewi na hawa wote kama wengi wamempa Karia, mjiulize pia hawajielewi kweli au waliona anastahili sahihi?

Acheni uchaguzi ufanyike nanyi mjipange badala ya kuwa walalaimishi tu.