Home news MAYELE ALIMCHUNGULIA MANULA KABLA HAJAMTUNGUA KWA MKAPA

MAYELE ALIMCHUNGULIA MANULA KABLA HAJAMTUNGUA KWA MKAPA


 MSHAMBULIAJI wa Yanga, Fiston Mayele ameweka wazi kuwa alimchungulia kwa mbali mlinda mlango Aishi Manula na kuona kwamba ametoka kidogo kulitanua goli jambo ambalo lilimfanya aamue haraka kupiga mpira alioupata kabla haujapoa wala kuzongwa na mabeki ili aweze kufunga.

Septemba 25, Simba ilipoteza mbele ya Yanga kwa kunyooshwa bao 1-0 ilikuwa kwenye mchezo wa Ngao ya Jamii na mtupiaji alikuwa ni Mayele aliyefunga bao hilo kipindi cha kwanza kwa shuti kali la mguu wake wa kulia.

Raia huyo wa Dr. Congo ni ingizo jipya ndani ya Yanga ambapo aliibuka hapo wakati wa usajili wa dirisha kubwa na amekuwa gumzo kutokana na uwezo wake kuwa mkubwa uwanjani.


Nyota huyo amesema:”Kabla sijaupiga ule mpira niliopewa na Mussa, (Farid) tayari nilimuona kipa wa Simba, Aishi Manula akiwa amesogea kupunguza goli hivyo akili ikaniambia niuunganishe na nisitulize kwani ningempa kipa nafasi ya kujipanga na mabeki kunizonga.

“Hivyo nikaunganisha moja kwa moja nikafanikiwa kufunga ninashukuru katika hilo. Ninafurahi kuifunga Simba kwa kuwa ni moja ya jukumu langu la kufanya,” amesema.

Kwa sasa kikosi cha Yanga kipo Kagera kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo wa Ligi Kuu Bara dhidi ya Kagera Sugar unaotarajiwa kuchezwa kesho, Uwanja wa Kaitaba.

Mayele ni miongoni mwa nyota wa Yanga ambao wapo Kagera kwa ajili ya maandalizi ya mchezo huo wa ufunguzi kwao kwa msimu wa 2021/22.

SOMA NA HII  GONJWA LA AJABU LAMKUMBA KIUNGO WA YANGA