Home Habari za michezo SIMBA vs KAGERA SUGARA: PABLO AFUNGUKA KUTOJUA CHOCHOTE KUHUSU UBINGWA WA LIGI...

SIMBA vs KAGERA SUGARA: PABLO AFUNGUKA KUTOJUA CHOCHOTE KUHUSU UBINGWA WA LIGI KUU…


Kagera Sugar wako jijini Dar es Salaam tayari kwa mechi dhidi ya Simba huku benchi la ufundi la timu hiyo likisisitiza kwamba hakuna namna kwenye mchezo wa leo dhidi ya wenyeji Simba.

Kagera Sugar itakuwa ugenini kwenye uwanja wa Mkapa mchezo wa mzunguko wa 22 wa Ligi Kuu utakaochezwa saa moja usiku.

Makocha wa timu hizo, wameuzungumzia mchezo huo, huku kocha msaidizi wa Kagera, Buberwa Bilikesi akisisitiza kuwa hakuna namna nyingine zaidi ya kurudi na pointi tatu mjini Bukoba.

“Morali ya kikosi chetu na jinsi msimamo wa Ligi ulivyo, hakuna namna nyingine zaidi ya kuhitaji pointi tatu,” amesema.

Kocha huyo amejinasibu kuwa timu yao ni miongoni mwa zenye matokeo mazuri ya ugenini msimu huu hivyo wanakwenda kuiendeleza kwa Simba.

“Kila gemu tuna plani yetu, kwa gemu ya Simba pia hiko hivyo na tuna malengo ya kucheza mashindano ya kimataifa msimu ujao, ili tufike huko lazima tushinde hivyo hakuna namna nyingine zaidi ya kushinda,” amesema.

Kocha Pablo Franco wa Simba amesisitiza kutaka ushindi kwenye mechi hiyo huku akibainisha kuwa safari ya ubingwa wa msimu huu itajulikana baadae.

“Naamini kesho ‘leo’ tutapambana kupata pointi tatu,  Kagera ni timu nzuri, ila tuna imani ya kuondoka na pointi tatu,” amesema.

Kuhusu harakati za ubingwa kwa timu yao kufuatia matokeo ya sare tatu mfululizo ya Yanga ambayo inaongoza kwenye msimamo, Pablo alisema bingwa atajulikana mwishoni mwa msimu.

“Hakuna kitu ambacho hakiwezekani, tunacheza Ligi kutafuta matokeo mazuri, nani atakuwa bingwa itajulikana baada ya mechi zetu kumalizika, nini kitatokea kwa sasa hatujui,” amesema.

Mechi ya mzunguko wa kwanza ilimalizika kwa Kagera Sugar kushinda bao 1-0 katika uwanja wa Kaitaba likifungwa na Hamis Kiiza.

SOMA NA HII  JEMBE JIPYA YANGA LAPANIA KUFANYA KWELI