Home Habari za michezo BAADA YA KUFUNGWA MAGOLI YA KIZEMBE…’NDOA’ YA SHIKHALO NA MTIBWA YAVUNJIKA RASMI…

BAADA YA KUFUNGWA MAGOLI YA KIZEMBE…’NDOA’ YA SHIKHALO NA MTIBWA YAVUNJIKA RASMI…

Aliyekuwa kipa wa Mtibwa Sugar, Faruk Shikhalo amekubali yaishe baada ya kusitisha mkataba na klabu hiyo kisha kutimkia kwao Kenya.

Hatua hiyo inakuja kufuatia kipa huyo kuwa katika lawama kwa mashabiki na hata baadhi ya viongozi wa klabu hiyo kwa madai ya kuyumba kwa kiwango chake.

Akizungumza akiwa kwao Kenya kwa njia ya simu Shikhalo amesema amelazimika kuchukua uamuzi huo baada ya kuona mambo hayaendi sawa.

Amesema amechukua uamuzi huo Novemba 14 siku moja baada ya mchezo wa timu hiyo dhidi ya Azam ambao ukimalizika kwa Mtibwa kupokea kipigo cha mabao 4-3.

Katika mabao hayo 4 Shikhalo aliruhusu mabao 3 katika kipindi cha kwanza tu kisha kutolewa mara baada ya kipindi hicho kumalizika.

“Nimeshaondoka Tanzania nipo nyumbani Nairobi,niliona tufikie uamuzi huo, mara tu baada ya Ile mechi na Azam ambayo tulipoteza,kesho yake nikaandika barua ya kusitisha mkataba,”amesema Shikhalo ambaye ni kipa wa zamani wa KMC na Yanga.

“Kuna mambo niliona hayako sawa na huwa sipendi kukabiliana na mambo magumu ambayo nayaona yako nje ya uwezo wangu,katika kulinda heshima yangu na hata Mtibwa pia nikaona tufikie sehemu ya kuachana kwa amani.

“Niliona lawama ziko sana upande wangu na hakuna ambaye hata anataka kujua uhalisia ukoje, yako mengi lakini itoshe kwangu kusema hivyo na nawatakia kila la kheri wachezaji wenzangu na timu kwa ujumla katika kuendelea kwa ligi,”

SOMA NA HII  MASTAA HAWA WATATU YANGA KUFUNGA USAJILI