Home Habari za michezo TAKWIMU ZINAONGEA….YANGA WAKIKAZA WANATOBOA ROBO FAINAL SHIRIKISHO CAF…

TAKWIMU ZINAONGEA….YANGA WAKIKAZA WANATOBOA ROBO FAINAL SHIRIKISHO CAF…

Tetesi za Usajili Yanga

Yanga inaonekana kutishia maisha ya timu nyingine kwenye kundi lake la Kombe la Shirikisho Afrika kutokana na rekodi zake ambazo zinatofautiana na wapinzani wake.

Yanga imekuwa timu bora kwa misimu miwili sasa baada ya kufanya usajili kabambe na kwenye michezo zaidi ya 50 ya ligi wamepoteza mchezo mmoja tu.

Juzi makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika yalipangwa na Yanga kuwekwa kundi moja na TP Mazembe ya DR Congo, Us Monastir ya Tunisia na Real Bamako ya Mali.

Yanga itaanzia ugenini kuvaana na Monastir Februari 12, watarundi nyumbani kuvaana na Mazembe Februari 19, watakwenda Mali kuwafuata Bamako Februari 26, Machi 8 watarudi Dar kuvaana na Bamako, Machi 19 watawakaribisha watamalizia ugenini kwa Mazembe Aprili 2.

Pamoja na Yanga kutokuwa na rekodi kubwa kwenye michuano hiyo, lakini takwimu zinaonyesha kuwa ndiyo timu pekee ambayo inaweza kufanya vizuri msimu huu kwenye kundi lake kuliko nyingine.

Katika misimamo ya ligi ya timu zote ambazo zipo kwenye kundi hilo, Yanga ndiyo timu pekee ambayo ipo kileleni kwenye ligi yake lakini ikiwa na takwimu nzuri za mabao ya kufunga na kufungwa.

Wakati Yanga ikiwa kileleni na pointi 38, baada ya michezo 15, wamepoteza mchezo mmoja tu na kutoka sare michezo miwili, wanaonekana pia kuwa na wastani mzuri wa mabao ya kufunga ambayo ni 27 na kufungwa 8.

Hawa ni tofauti na Mazembe, ambao wapo katika nafasi ya nne kwenye Ligi Kuu ya nchini kwao wakiwa wameshacheza michezo nane, pamoja na kwamba michezo yao ni michache kuliko ya Yanga, takwimu zimeshaonyesha kuwa wamepoteza mchezo mmoja na kutoka sare mitatu wakiwa wanaonekana hawana kasi kwenye ufungaji baada ya kufunga mabao 15 tu na kufungwa mabao manne, ligi yao inaongozwa na Lupopo ambao wamewazidi kwa pointi saba.

Mbali na Mazembe, kule nchini Tunisia ambapo inatoka timu ya Monastir ligi yao ipo kwenye makundi mawili, ambapo kundi lao ni B wakiwa wanashika nafasi ya tatu baada ya kukusanya pointi kumi kwenye michezo mitano, wametoka sare mmoja na kupoteza mmoja.

Hawana nguvu ya kufunga mabao kutokana mechi kwenye mchezo mmoja na wakiwa wamefunga mabao matano tu katika michezo mitano wastani wa bao moja kwenye kila mchezo, lakini wameruhusu kufungwa mabao matatu, hii inaonyesha kuwa siyo timu bora kwenye kulinda na haina ubora kufunga mabao, wameachwa kwa pointi mbili na vinara Ben Guerdane wenye pointi 12, kitakwimu ni sahihi kwamba hawawezi kuwatikisa Yanga.

Bamako wakiwa wameshacheza michezo sita, wenyewe wanaonekana wakiwa hawajapoteza mchezo kwenye ligi yao, wakiwa wametoka sare mara mbili, lakini siyo bora kwenye kufunga baada ya kutupia mabao tisa kwenye michezo hiyo na kuruhusu nyavu zake kutikiswa mara tatu.

Wastani huu unaonyesha kuwa ni timu ambayo Yanga wanaweza kuifunga, wastani wa Yanga kwenye kila mchezo tofauti takwimu zinaonyesha kuwa wana wastani wa kufunga mabao mawili.

Hali halisi inaonyesha kuwa kama Yanga watajipanga vyema wanaweza kumaliza nafasi kwanza kwenye kundi lake na kuwaacha wengine wapambanie nafasi moja iliyobaki.

Kocha Mkuu wa Yanga, Nasreddine Nabi alisema wanaingia kwenye ushindani kwa kuwaheshimu wapinzani huku akiwashtua washambuliaji wao kuhakikisha wanatumia kila nafasi watakazozipata.

Alisema ni kundi ambalo kwa hesabu kila timu inanafasi lakini wao wanajiandaa kuhakikisha wanaipigania timu iweze kutinga hatua inayofuata huku akisisitiza kuwa uwanja wa nyumbani ndio muhimu zaidi kupata matokeo kabla ya kwenda kujaribu bahati ugenini.

“Ushindi kwenye uwanja wa nyumbani na idadi kubwa ya mabao utatusaidia kuweza kujihakikishia nafasi ya kutinga hatua inayofuata na kuupata kwenye ardhi ya ugenini inawezekana lakini kipaumbele ni nyumbani zaidi kwasababu kila timu inahitaji matokeo ili kuweza kuongoza kundi na kupata nafasi ya kusonga,”

“Tulishindwa kutumia vyema uwanja wa nyumbani kwenye hatua ya Ligi ya Mabingwa na hata mchezo wa Kombe la Shirikisho nyumbani hatukuwa vyema hatutaki kurudia makosa kwenye hatua hii japo lolote linaweza kutokea nyumbani na ugenini kuweza kupata matokeo,” alisema Nabi.

SOMA NA HII  PAMOJA NA KUPATA USHINDI JANA...NABI AFUNGUKA ALIVYOBANWA NA KUTUMIA NJIA MBADALA...