Home Habari za michezo WAKATI ONYANGO AKIZIDI ‘KUWADINDIA….MABOSI SIMBA WAPANIA KUPINDUA MEZA KIBABE …

WAKATI ONYANGO AKIZIDI ‘KUWADINDIA….MABOSI SIMBA WAPANIA KUPINDUA MEZA KIBABE …

Tetesi za Usajili Simba

Mabosi wa Simba SC wameweka wazi kuwa maboresho yatakayofanywa kwenye kikosi hicho kwa msimu wa 2023/24 ni makubwa yenye malengo ya kuimarisha kikosi kitakachokuwa na uwezo wa kutwaa mataji.

Timu hiyo chini ya Kocha Mkuu, Roberto Oliveira, Raia wa Brazil imegotea nafasi ya pili kwenye ligi huku ikishuhudia Young Africans wakitwaa ubingwa wa ligi kwa mara ya pili mfululizo.

Katika anga za kimataifa imegotea Robo Fainali Ligi ya Mabingwa Afrika huku watani zao wa jadi Young Africans kwenye Kombe la Shirikisho Barani Afrika wakiwa washindi wa pili baada ya kucheza Fainali.

Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi, Salim Abdallah ‘Try Again’ amesema kuwa kwa makosa ambayo wamepitia msimu wa 2022/23 ni somo kwao.

“Makosa ambayo yametokea kwa msimu ambao umeisha ni somo kwetu na tumeona pale ambapo tulikwama kufanikiwa hasa kwa wachezaji ambao tulikuwa nao pamoja na wale ambao tuliwaacha.

“Kikubwa kwa wakati ujao ni kuona tunakuwa na timu bora itakayotufanikishia malengo yetu ya kutwaa mataji kwani hilo ndilo jambo ambalo tunalitarajia na tunaamini itakuwa hivyo.”

Tayari kikosi hicho kimeanza kupitisha panga kwa wachezaji wao ikiwa ni pamoja na Erasto Nyoni, Jonas Mkude, Augustine Okrah, Nelson Okwa, Beno Kakolanya na Victor Akpan.

ONYANGO AZIDI KUDINDA..

Katika hatua nyingine mastaa wa kikosi cha Simba wameitwa jijini Dar es Salaam kwa ajili ya vipimo vya afya vitakavyofanyika wiki ijayo, lakini taarifa mbaya ni kwamba beki Mkenya, JoashOnyango amezidi kukomaa kwa kuandika barua nyingine tena ya kusisitiza aachiwe asepe kwenda klabu nyingine.

Msimamo wa beki huyo wa zamani wa Gor Mahia, unazidi kuwapa wakati mgumu mabosi wa klabu hiyo ambao kwa sasa wanabanguliwa kichwa na sakata la kiungo Ismael Sawadogo.

Sawadogo anahitaji Sh 700 milioni ili kuvunjiwa mkataba atimke zake, lakini kibaya zaidi ni kwamba Onyango naye ameshikilia msimamo wake kwa kuandika barua ya kutaka kuondoka klabuni hapo, wakati mabosi hao wakiwa hawajapata mbadala wake kikosini.

“Onyango ametuma barua nyingine ya maombi kutaka kuondoka ndani ya timu kutokana na kile kilichoelezwa anaamini usajili wa beki mpya utazidi kuongeza changamoto kwake ya kupata nafasi ya kucheza kutokana na viongozi kukosa imani naye,” kilisema chanzo makini kutoka ndani ya Simba na kuongeza;

“Ameomba mazungumzo yafanyike ili aweze kuondoka kwenda kujaribu changamoto nje ya Simba.” Mbali na Onyango, inaelezwa pia beki mwingine wa kati Keneddy Juma amegoma kuongeza mkataba mwingine pamoja na kuitwa mezani kwa madai kwamba anahitaji kupata timu ambayo itampa nafasi ya kucheza mara kwa mara, huku akihusishwa na klabu ya Singida Big Stars.

“Simba ipo kwenye nyakati ngumu kuopambana kuhakikisha zinabaki na wachezaji hao wawili kwasababu timu ina mashindano mengi tunaamini wote watapata muda wa kucheza,” kilisema chanzo hicho kilichohifadhiwa jina.

“Pia eneo la beki sio la kuwa na imani ya moja kwa moja kwenye usajili mpya tutahitaji kufanya majaribio na kama tutaridhishwa na uwezo wa usajili mpya ndio tutakuwa na chaguo sahihi hivyo ni ngumu kuwa na jibu la moja kwa moja kukubaliana na ombi la wachezaji wote wawili.” kilisisitiza chanzo hicho.

Akizungumzia suala la wachezaji kuanza kupima Afya alisema litakuwa ni zoezi la siku mbili, likianza Jumatano na kumalizika Jumanne ya mwezi huu, huku akisisitiza wachezaji wote wanatakiwa kuripoti haraka kambi ya timu hiyo iliyopo Dar es Salaam ikiwa ni maandalizi ya kambi ya msimu mpya nje ya nchi.

“Vipimo kila msimu unapoanza umekuwa ndio utaratibu wetu ili kufahamu afya za wachezaji wetu kabla ya kuanza kambi, hivyo tunatumaini ndani ya siku hizo mbili mambo yatakuwa yamekamilika na utaratibu wa kambi utafuata.” kilisema chanzo hicho.

Pamoja na uongozi kufanya siri lakini taarifa zinadai  kuwa timu hiyo inatarajia kuweka kambi Afrika Kusini.

SOMA NA HII  SIMBA: TUMEJIPANGA KUPATA USHINDI MBELE YA YANGA