Home Habari za michezo FT: YANGA 2-0 SINGIDA BIG STARS…..KWA MAKALI HAYA YA GAMONDI…SIMBA TAFUTENI SABABU...

FT: YANGA 2-0 SINGIDA BIG STARS…..KWA MAKALI HAYA YA GAMONDI…SIMBA TAFUTENI SABABU MAPEMA…

Habari za Yanga

MABAO mawili aliyoyafunga Maxi Nzengeli leo Ijumaa kwenye Uwanja wa Mkapa dhidi ya Singida Big Stars wa 2-0, yameifanya timu hiyo kuendelea kujikita kileleni mwa msimamo kwa kufikisha pointi 18 katika michezo saba iliyocheza.

Yanga imekaa kileleni huku watani zao Simba kesho Jumamosi watakuwa na kibarua dhidi ya Ihefu FC kutoka Mbarali mechi ambayo pia itachezwa Uwanja wa Mkapa. Simba yenyewe ina pointi 15 ikiwa imecheza mechi tano.

Huu ni ushindi wa tatu mfululizo tangu wafungwe na Ihefu, waliifunga Geita mabao 3-0, ushindi wa mabao 3-2 dhidi ya Azam na leo kuifunga SBS.

Katika mechi ya leo, Yanga ilipata mabao yake mawili kipindi cha kwanza kupitia kwa kiungo mshambuliaji Maxi aliyeanza kucheka na nyavu dakika ya 30 kwa kichwa akimalizia krosi ya Atoula Yao, na dakika nane baadae, akapiga bao la pili kwa shuti kali nje kidogo ya boksi la 18 la Singida na kuzama moja kwa moja nyavuni.

Baada ya bao hilo la pili, Singida ililazimika kufanya mabadiliko ya lazima ikimtoa kipa wake, Benedict Haule aliyeumia na nafasi yake kuchukuliwa na Ibrahim Kashindi.

Licha ya Yanga kuendelea kulishambulia mara kwa mara bao la Singida lakini ilishindwa kuongeza bao na dakika 90 kumalizika ikiongoza kwa 2-0.

Kipindi cha pili kilianza kwa timu zote kufanya mabadiliko ambapo Yanga ilimtoa Mudathiri Yahya na kuingia Salum Abubakari ‘Sure Boy’ huku Singida ikiwaingiza Deus Kaseke na Francy Kazady waliochukua nafasi za Habibu Kyombo na Duke Abuya na dakika ya 58 Singida ilifanya mabadiliko mengine kwa kumuingiza Moriss Chuku aliyechukua nafasi ya Bruno Gomes.

Baada ya mabadiliko hayo, timu zote iloendelea kushambuliana kwa kupokezana huku Yanga ikiongoza na dakika ya 72 iliwaingiza Kennedy Musonda na Makudubela ‘Skudu’ mchezoni kuchukua nafasi za Hafiz Konkoni na Zuozuoa Pacome na Singida ikajibu mapigo kwa kumuingiza Meddie Kagere na kutoka Aziz Andambwile.

Maxi ambaye amekuwa kwenye kiwango kizuri msimu huu mabao hayo yanamfanya kufikisha matano katika Ligi Kuu Bara sawa na Jean Baleke wa Simba huku wote wakiwa chini ya Stephano Aziz Ki wa Yanga anayeongoza akiwa na sita.

Watatu hao, kila mmoja ana nafasi ya kumpindua mwenzake katika orodha hiyo ya ufungaji kwani mechi ijayo wote watakutana ambapo, Azizi Ki na Nzengeli watakuwa na Yanga huku Baleke akiwa na Simba, katika Dabi ya Novemba 5, mwaka huu.

Ukiachana na hayo, Yao ameendelea kujikita kileleni mwa msimamo wa kutoa pasi za mwisho ‘Asisti’ kwani krosi yake iliyozalisha bao la kwanza imekuwa asisti ya nne kwake msimu huu.

Mechi hiyo imekuwa ya tatu mfululizo kwa Yanga kuifunga Singida kwenye ligi tangu imepanda daraja msimu uliopita kwani katika mechi mbili zilizopita ilianza kwa kushinda 4-1, Novemba 17 mwaka jana kisha kuchapwa 2-0, Mei 4, mwaka huu kwenye Uwanja wa Liti mkoani Singida.

SOMA NA HII  PAMOJA NA YANGA KUFANYA VIZURI...GSM WASHINDWA KUJIZUA...WALIA KUPATA HASARA..WAITAJA LA LIGA..