Mabingwa watetezi wa Kombe la FA, Yanga SC, wataanza safari yao ya kutetea taji kwa kucheza dhidi ya Copco FC kutoka Mwanza, inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza (First League). Kwa upande wa Simba SC, wao wamepangwa kuvaana na Kilimanjaro Wonders katika hatua ya 64 bora ya michuano hiyo.
Michezo hiyo inatarajiwa kuanza mwanzoni mwa mwezi ujao, ambapo timu zote mbili, Yanga na Simba, zimepangiwa wapinzani kutoka madaraja ya chini, hali ambayo pia inaonekana kwa klabu nyingine za Ligi Kuu Bara.
Hii itakuwa mara ya kwanza kwa Yanga kukutana na Copco FC, hali sawa na Simba kukutana na Kilimanjaro Wonders. Singida Black Stars, chini ya kocha Patrick Aussems, watacheza dhidi ya Magnet FC, wakati Azam FC watachuana na Iringa SC.
Akiongelea droo hiyo ambayo ilisimamiwa na Meneja Mashindano wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Tanzania (TFF), Baraka Kizuguto, nyota wa zamani wa Simba na Yanga Danny Mrwanda alisema anaamini hii ni fursa kwa timu za madaraja ya chini kujipima ubavu wa kumudu kukabiliana na timu za madaraja ya juu.
“Zipo timu za madaraja ya chini ambazo hupambana na kufika mbali katika michuano ya FA, binafsi huwa nachukulia mashindano haya kama nafasi yao ya kujipima kabla ya kufika madaraja ya juu, inasaidia kuona kwa namna gani mnatakiwa kuongeza nguvu,” alisema nyota huyo.
Kwa upande wake, kocha wa Singida Black Stars,Aussems alisema,”Ni droo nzuri kwa upande wangu, kilichopo kwanza ni kucheza hatua kwa hatua michezo iliyopo mbele yetu kwenye ligi kabla ya mchezo huo, itakuwa nafasi nyingine kwetu.”