Home Habari za michezo NI VITA YA CHIPO, MAXIME LIGI KUU BARA

NI VITA YA CHIPO, MAXIME LIGI KUU BARA

18
0

MIEZI 10 na siku 9 imepita kufikia leo Januari 21, 2026 na tunakwenda kushuhudia tena mtanange baina ya Mtibwa Sugar dhidi ya Mbeya City, huku safari hii ikiwa ni katika Ligi Kuu Bara. Uwanja wa Jamhuri uliopo Dodoma, utaamua vita hiyo ya makocha wawili, Yusuf Chipo na Mecky Maxime kuanzia saa 10:00 jioni.

Timu hizo zilizomaliza nafasi mbili za juu katika msimamo wa Ligi ya Championship msimu uliopita 2024-2025 na kukata tiketi ya moja kwa moja kurejea Ligi Kuu Bara, zinakutana kwenye mechi ya ligi kila moja ikihitaji matokeo mazuri.

Kwa Mbeya City inayonolewa na Mecky Maxime, inabaki kuwa deni kubwa kwao kwani msimu uliopita dhidi ya Mtibwa Sugar zilipokutana Championship, haikupata ushindi zaidi ya kuambulia pointi moja zilipotoka 0-0, Februari 9, 2025 kwenye Uwanja wa Sokoine, Mbeya ikiwa ni mechi ya raundi ya 18 duru la pili.

Kabla ya hapo, Mtibwa ilishinda nyumbani mabao 2-0 dhidi ya City, Oktoba 5, 2024 ikiwa ni mechi ya raundi ya tatu.

Mwisho wa msimu huo, ilishuhudia Mtibwa Sugar ikimaliza kinara wa Ligi ya Championship ikifikisha pointi 71 baada ya kucheza mechi 30, ikishinda 22, sare tano na kupoteza tatu, huku ikifunga mabao 58 na nyavu zake kutikiswa mara 18.

City ilikuwa ya pili na pointi 68, ikishuka dimbani mara 30, ikishinda mechi 20, sare nane na kupoteza mbili, ikifunga mabao 68 na kuruhusu 26.

Timu hizo baada ya kwenye Ligi ya Championship Mtibwa Sugar kufanya vizuri, City ikaenda kulipa kisasi Machi 13, 2025 katika mechi ya hatua ya 16 bora ya Kombe la Shirikisho (FA) iliposhinda 2-1 na kufuzu robo fainali, ikaenda kukwaa kisiki cha Simba. Hiyo ndiyo ilikuwa mara ya mwisho City kucheza dhidi ya Mtibwa.

Msimu huu Ligi Kuu, Mtibwa Sugar inayonolewa na Yusuf Chipo, ipo juu ya City tena kwa tofauti kubwa ya pointi na nafasi.

Mtibwa kabla ya mechi mbili zilizochezwa jana, ilikuwa nafasi nane ikikusanya pointi 11 baada ya kucheza mechi tisa, ikishinda mbili, sare tano na kupoteza mbili, ikifunga mabao matano na kuruhusu idadi hiyo.

City haijaanza vizuri sana msimu huu kulinganisha na mpinzani wake kwani inakamata nafasi ya 13 ikikusanya pointi nane zilizotokana na kushinda mechi mbili na sare mbili, ikipoteza nane. Imefunga mabao saba na kuruhusu 13 ikishuka dimbani mara kumi.

Rekodi zinaonyesha kuwa, msimu wa mwisho 2022-2023 timu hizo kukutana Ligi Kuu Bara kabla ya kila moja kushuka kwa wakati wake, City ilifanya vizuri dhidi ya Mtibwa ikikusanya pointi nne baada ya kutoka 2-2, kisha ikashinda bao 1-0.

Tangu msimu wa 2013-2014, timu hizo zimekutana mara 20, Mtibwa Sugar ikishinda sita, City nayo imeibuka na ushindi mara tano, huku sare zikiwa tisa.

Jumla ya mechi 23 zimechezwa baina ya timu hizo katika Ligi Kuu (20), Championship (2) na Kombe la FA (1), huku ikishuhudiwa mara tano pekee zikitoka uwanjani bila ya nyavu kutikiswa, hivyo zinapokutana, ishu ya kufunga bao ipo kwa asilimia kubwa.

Kocha Mecky Maxime, huu ni mtihani wake wa kwanza tangu akabidhiwe mikoba ya kuinoa timu hiyo Desemba 7, 2025 akichukua nafasi ya Malale Hamsini.

Maxime ana mtihani wa kuhakikisha City inapata matokeo mazuri kwani mechi yano za mwisho, imekusanya pointi moja, ilipotoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya JKT Tanzania, baada ya hapo ikafungwa na Mashujaa (1-0), ikachapwa 2-0 na Coastal Union, kisha ikapokea kipigo cha 1-0 kutoka Namungo, ikahitimisha na kufungwa 3-0 dhidi ya Simba.

Mtibwa mechi tano za mwisho imekusanya pointi sita ikipoteza mechi moja pekee dhidi ya Yanga ilipofungwa 2-0. Baada ya hapo, matokeo yalikuwa hivi; KMC 0-0 Mtibwa, Mtibwa 2-1 TRA, JKT 0-0 Mtibwa na Simba 1-1 Mtibwa.