Home Habari za michezo
0

Leicester, England: Leicester City imeshuka daraja kwa mara ya pili mfululizo hadi League One, takribani muongo mmoja tu baada ya kutwaa ubingwa wa Ligi Kuu England (Premier League).

Kikosi hicho cha Gary Rowett kilihitaji matokeo yasiyotarajiwa ili kubaki katika Championship lakini kikatoka sare ya mabao 2-2 dhidi ya Hull City, kikiwa kimeingia kwenye mchezo huo kikiwa nyuma kwa pointi nane kutoka eneo salama huku kukiwa na mechi tatu pekee zilizobaki.

Timu ya Hull iliyokuwa ikipigania nafasi za mchujo (play-offs) ilithibitisha kushuka kwa Leicester katika Uwanja wa King Power. Leicester walikuwa nyuma kwa bao 1-0 kipindi cha kwanza kufuatia bao la Liam Millar, lakini walipata matumaini pale Jordan James alipofunga penalti dakika ya 52, na dakika mbili baadaye Luke Thomas akaongeza bao la pili.Ushindi wa kwanza katika michezo nane ungeweza kuipa Leicester nafasi ya kupambana hadi mechi mbili za mwisho wa msimu, lakini bao la 15 la Ollie McBurnie msimu huu lilisawazisha na hawakuweza kupata bao la ushindi.Leicester walianza msimu wakiwa miongoni mwa timu zilizokuwa zikipewa nafasi kubwa ya kupanda daraja baada ya kushuka kutoka Premier League mwaka uliopita.Marti Cifuentes, aliyeteuliwa kuwa kocha majira ya kiangazi, alifutwa kazi Januari wakati timu ikiwa nafasi ya 14 kwenye msimamo wa Championship, pointi sita nyuma ya nafasi za play-offs.

Andy King alisimamia timu kwa muda mfupi na kushuhudia vipigo vinne kabla ya Gary Rowett kuteuliwa Februari.

Tangu hapo, Leicester walishinda mechi moja tu kati ya 11 walizocheza, na kuingia katika eneo la kushuka daraja kabla ya kupoteza kabisa matumaini ya kujinasua.

Matumaini yao yalidorora zaidi mapema mwezi huu baada ya rufaa yao kupinga kupokwa pointi sita kukataliwa. Adhabu hiyo iliwekwa Februari na kamati huru baada ya kukiuka kanuni za kifedha za Premier League zinazohusiana na msimu wa 2023-24 walipokuwa Championship.

Mashabiki wameonyesha hasira kwa wamiliki wa klabu na wachezaji kufuatia msimu mbaya uliosababisha kushuka daraja kwa mara ya tatu ndani ya misimu minne.

Kiungo Harry Winks, anayeripotiwa kulipwa pauni 90,000 kwa wiki, alionekana kugombana na mashabiki alipokuwa akielekea kwenye basi la timu kufuatia kipigo cha 1-0 dhidi ya Portsmouth mwishoni mwa wiki, matokeo yaliyowaweka hatarini timu hiyo.Kushuka kwa Leicester hadi daraja la tatu ni mara ya pili tu katika historia ya klabu hiyo, na kunakuja miaka kumi baada ya ushindi wao wa kushangaza wa ubingwa wa Premier League.Kabla ya mechi dhidi ya Hull, Leicester walitangaza kuwa wataadhimisha miaka 10 tangu ushindi huo kwa mechi ya hisani itakayokusanya fedha kupitia taasisi ya Vichai Srivaddhanaprabha.

Mwenyekiti wa klabu hiyo, Aiyawatt Srivaddhanaprabha, ambaye baba yake marehemu Vichai alisimamia mafanikio ya ubingwa huo, aliomba radhi kwa mashabiki kufuatia kushuka daraja hadi League One.“Kwa mashabiki wetu, kushuka daraja hadi League One sasa kumethibitishwa. Kama mwenyekiti, jukumu hilo liko kwangu. Hakuna visingizio,” ilisema taarifa hiyo.“Tumeonja mafanikio makubwa kabisa na sasa tumefikia hali ya chini zaidi, na maumivu haya yanatugusa sote. Ninaomba radhi kwa kukatisha tamaa tuliyosababisha.“Ninaelewa hisia kali za mashabiki wetu, na hatuchukulii kirahisi sapoti yenu, hasa katika nyakati kama hizi. Sasa tunalenga hatua inayofuata.“Tutachukua maamuzi muhimu ili kuisogeza mbele klabu, tukifanya kazi pamoja kujenga upya, kuboresha, na kurejesha viwango vinavyotarajiwa kwa Leicester City.“Lengo letu ni wazi kujibu kwa nguvu na kupambana kuirudisha klabu hii juu tena. Tutakabiliana na hali hii moja kwa moja. Tutaendelea kupambana. Pamoja.”