Pamoja na matokeo ya mechi hizo, hakukuwapo na malalamiko kutoka kwa wachezaji, timu wala mashabiki na hivyo, msomi huyu wa shahada ya ualimu katika masomo ya Hisabati na Fizikia ni mmoja wa waamuzi ambao wakipewa mechi hiyo ya dabi, huenda wakawa na imani naye.
SIFU AMON
Anatoka jijini Mbeya na amekuwa na uwezo mkubwa katika kusimamia mechi za ligi na Kombe la Shirikisho la CRDB, akizingatia sheria na kanuni za soka.
Hadi sasa amesimamia mechi 10 na zote hakujatokea malalamiko wala kuitwa na Kamati ya saa 72 na licha ya kutokuwa na uzoefu mkubwa akianza kazi hiyo mwaka jana, ameonyesha nidhamu, akiendana na kasi ya mechi na hivyo kuifanya kazi yake kuwa nyepesi.
Mechi alizochezesha ni KMC dhidi ya Singida Black Stars, JKT Tanzania dhidi ya Mtibwa Sugar, Simba dhidi ya Mtibwa Sugar, Mtibwa Sugar dhidi ya Coastal Union na Azam dhidi ya TRA United.
Nyingine ni Namungo dhidi ya JKT Tanzania, Pamba dhidi ya Yanga kwa upande wa Ligi Kuu, huku za kombe la shirikisho ni Namungo dhidi ya Kagera Sugar na Simba dhidi ya Dodoma Jiji hatua ya robo ya 16 bora.
Kutokana na kuaminiwa kwake na kuonyesha uwezo katika mechi hizo 10, zikiwamo kubwa, ni wazi akipewa mechi ya dabi ataimudu kwa dakika zote 90.
SAAD MROPE
Tangu alipomaliza kozi yake mwaka 2014 na kuanza kuliamsha mwaka 2015, amekuwa na ubora huku wadau na mashabiki wa soka wakikubali shughuli yake.
Mrope ambaye pia ni inspekta wa Jeshi la Polisi, Dodoma, pia ni msomi mwenye Shahada ya Elimu ya Viungo na Sayansi ya Michezo na anayamudu majukumu yake vyema nje na ndani ya uwanja.
Msimu huu amechezesha mechi saba bila ‘makosa ya kibinadamu’ na amekuwa kipenzi cha mashabiki kutokana na kutenda haki muda wote bila upendeleo wala kuonea upande wowote katika mechi.
Mechi zaka hadi sasa raundi 19, ni Coastal Union dhidi ya JKT Tanzania, Mbeya City dhidi ya Tanzania Prisons, Pamba Jiji dhidi ya Azam FC, Yanga dhidi ya JKT Tanzania, TRA United dhidi ya Namungo, Yanga dhidi ya Tanzania Prisons na Fountain Gate dhidi ya Simba.
KAULI ZA WADAU
Mdau wa soka kutoka mkoani Songwe, Moses Charles anasema kwa sasa waamuzi wengi wameonekana kuwa imara uwanjani kutokana na mamlaka za soka kutowafumbia macho wale wanaoboronga.
Anasema katika kukuza na kutanua wigo wa waamuzi, shirikisho la soka nchini linaweza kuwapa waamuzi ambao wanajitafuta na kuondoa dhana ya kuwapanga waliozoeleka.
“Kuna kipindi waliletwa waamuzi kutoka nje lakini siioni kama ni bora ilhali tunao waamuzi wenye uwezo na elimu, mtu akifanya vizuri apongezwe na kuaminiwa. Waamuzi chipukizi wanafanya vizuri,” anasema Charles.
“Mimi binafsi nashauri watafute waamuzi ambao hawana vinasaba vya Simba na Yanga, wanaotimiza wajibu wao kwa mujibu wa kanuni na sheria za soka bila kupendelea au kuonea, tumeona mara kadhaa maamuzi ya upande mmoja kwenye hizi dabi.”
Kwa upande wake, Yusuph Edson anasema wapo waamuzi wengi msimu huu wameonyesha uwezo na weledi katika kusimamia kanuni za soka akiomba uwezekano wa kuwapa nafasi ili kuonesha uwezo wao.
“Ligi si ya timu moja wala refa mmoja, tunaona hata kwa wenzetu Ulaya refa akiwa na sifa anapewa jukumu kuchezesha mechi yoyote, kwetu sisi tunaona kila mara mtu yuleyule, hii inaweza kutupa maswali mengi,” anasema Edson.