Home Habari za michezo YANGA KUWAKOSA WAWILI DABI

YANGA KUWAKOSA WAWILI DABI

0

WAKATI presha ya mchezo wa Kariakoo Dabi kwenye Fainali ya Kombe la Muungano ikizidi kupanda, benchi la ufundi la Yanga limetaja wachezaji wawili watakaowakosa.

Yanga itakutana na Simba kwenye mchezo huo wa Fainali ya Kombe la Muungano, itakayopigwa kesho Jumatano kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar kuanzia saa 2:15 usiku.

Kocha Mkuu wa Yanga, Pedro Goncalves amesema asilimia kubwa wachezaji wake wako sawa lakini kuna majeruhi wawili pekee wapya kikosini hapo.

Goncalves amewataja majeruhi hao kuwa ni beki Mohammed Hussein ‘Tshabalala’ na winga Buba Jammeh ambao wataukosa mchezo huo.

Kocha huyo amesema wachezaji hao wawili wanahitaji wiki moja kupona sawasawa kabla ya kurudi kwenye mazoezi.

“Tuna majeruhi ndio lakini wawili ndio ambao unaweza kusema watahitaji tubadilishe hesabu zetu, wa kwanza ni Tshabalala ambaye bado hajaanza mazoezi na mwingine Buba aliumia kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho la CRDB,” amesema Pedro.

“Hawa wawili watahitaji kama wiki moja ili waweze kuanza mazoezi, kwa hatua hiyo hatutaweza kuwa nao kwenye mchezo wa kesho dhidi ya Simba.

Aidha Pedro amesema kundi lingine la majeruhi ni lile la wachezaji watakaokaa nje kwa muda mrefu zaidi wakiwemo kipa Khomein Abubakar, beki Dickson Job na mshambuliaji Clement Mzize.

“Kuna wale ambao watakuwa nje kwa muda mrefu zaidi kama Job, Mzize na Khomein, hawa bado sana tutaendelea kuwakosa kutokana na wanaendelea kuimarika taratibu,” amesema.

Yanga na Simba baada ya mechi hiyo, timu hizo zitakutana tena Mei 3 mwaka huu katika Ligi Kuu Bara kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo, Dar es Salaam.