LONDON, ENGLAND: MANCHESTER City wanaonekana kushindwa katika jitihada za kubadilishiwa ratiba ya mechi dhidi ya Crystal Palace na Bournemouth, licha ya kukabiliwa na mzigo wa kucheza mechi tatu muhimu ndani ya siku saba.
Tatizo linaanzia pale ambapo mechi dhidi ya Bournemouth iliyopangwa kupigwa Mei 17, italazimika kuhamishwa kwa sababu ya fainali ya FA Cup dhidi ya Chelsea itakayochezwa siku moja kabla.
Zaidi ya hilo, Man City bado wana mechi ya kiporo dhidi ya Crystal Palace ambayo haijapangiwa tarehe mpya tangu ilipoahirishwa mwezi Machi. Pendekezo la sasa viongozi wa FA ni Palace kucheza ugenini Etihad, Mei 13, kisha Man City watasafiri kwenda kucheza na Bournemouth Mei 19.
Ratiba hiyo inawapa muda mdogo wa maandalizi, jambo lililosababisha City kutafuta suluhisho litakalowapa muda zaidi kabla ya fainali ya FA.
Kwa upande wao, wangependa pia kucheza kwanza na Bournemouth, kisha kumalizia msimu kwa mechi mbili za nyumbani ikiwemo dhidi ya Aston Villa siku ya mwisho.
Hata hivyo, angalau klabu tatu za Ligi Kuu England zimepinga wazo hilo. Kwa mujibu wa kanuni, siyo rahisi kubadilisha mpangilio wa mechi isipokuwa pale inapolazimika, na hivyo mechi ya nyumbani dhidi ya Palace inapaswa kuchezwa kabla ya safari ya Bournemouth.
Inaripotiwa kuwa baadhi ya klabu ziko tayari hata kuwasilisha malalamiko rasmi iwapo City wataruhusiwa kumaliza msimu kwa mechi mbili za nyumbani mfululizo.
Kwa sasa, dalili zinaonyesha kuwa City hawatakubaliwa mabadiliko wanayoyataka jambo linaloweza kuwaathiri katika mbio za mwisho wa msimu.