Home Habari za michezo ASHLEY YOUNG KUSTAAFU SOKA MWISHONI MWA MSIMU

ASHLEY YOUNG KUSTAAFU SOKA MWISHONI MWA MSIMU

0

IPSWICH, ENGLAND: ALIYEKUWA nahodha wa Manchester United na winga wa zamani wa timu ya taifa ya England, Ashley Young, ametangaza rasmi kuwa atatundika daruga mwishoni mwa msimu huu, akihitimisha safari ya kipekee ya miaka 23 ndani ya soka la kulipwa.

Young (40), ambaye kwa sasa anaitumikia Ipswich Town inayoshiriki Championship, amekuwa akisumbuliwa na jeraha la nyonga lililomuweka nje ya uwanja tangu mwezi Januari.

Katika taarifa yake ya hisia, Young ameeleza kujivunia mafanikio makubwa aliyoyapata tangu alipoanza soka la kulipwa mwaka 2003.

“Najivunia sana na kujiona mwenye bahati kufikia kila kitu nilichopata kwenye kazi yangu. Kwa miaka 23 iliyopita, nimeishi ndoto yangu,” amesema Young.

Ameongeza kuwa, kwa sasa nguvu zake zote amezielekeza kuisaidia Ipswich kufuzu kurejea Ligi Kuu ya England (Premier League) katika mchezo wa mwisho dhidi ya QPR.

Young alianza safari yake ndani ya Watford kabla ya kujiunga na Aston Villa mwaka 2007, ambapo kiwango chake bora kilimvutia Sir Alex Ferguson.

Mwaka 2011, alijiunga na Manchester United kwa ada ya pauni milioni 17. Akiwa Old Trafford, alicheza jumla ya mechi 261 na kuwa miongoni mwa wachezaji waliobeba taji la mwisho la Premier League la United msimu wa 2012-13. Kutokana na uongozi wake, aliteuliwa kuwa nahodha wa klabu hiyo mwaka 2019.

Mbali na soka la England, Young aling’ara nchini Italia akiwa na Inter Milan, ambapo aliisaidia klabu hiyo kutwaa taji la Serie A msimu wa 2020-21 chini ya kocha Antonio Conte. Baadaye alirejea Aston Villa, akapita Everton, na hatimaye kujiunga na Ipswich Town msimu uliopita.

Katika ngazi ya kimataifa, Young aliichezea England mara 39 kati ya mwaka 2007 na 2018, akiwakilisha “Three Lions” kwenye michuano mikubwa ya Euro 2012 na Kombe la Dunia 2018 nchini Urusi.

Kocha wa Ipswich, Kieran McKenna, ambaye pia alifanya kazi na Young ndani ya Manchester United, amemsifu mchezaji huyo kwa weledi wake.

“Imekuwa heshima kufanya naye kazi. Ubora wake umekuwa na athari kubwa kwa vijana wetu msimu huu,” amesema McKenna.

Ashley Young anaondoka uwanjani akiacha alama ya mchezaji aliyeweza kubadilika kutoka winga hatari na kuwa beki wa pembeni mwenye nidhamu ya hali ya juu.