Home Habari za michezo IBRA CLASS, MAPAMBANO YA NANI MKALI SASA NO

IBRA CLASS, MAPAMBANO YA NANI MKALI SASA NO

0

BONDIA wa kulipwa wa Tanzania, Ibrahim Mgender maarufu kama Ibra Class, ameweka malengo ya kushinda mataji makubwa ya kimataifa baada ya kutwaa mikanda miwili ya Kimataifa ya uzito wa super featherweight ya Baraza la Ndondi Duniani (WBC), Aprili 25, 2026 mjini Bangkok, Thailand.

Class alionyesha ubabe mkubwa katika pambano lililofanyika kwenye Uwanja wa World Siam, akimchapa bondia wa Thailand, Kritiphak Duangnut kwa TKO raundi ya tano kwenye marudiano yao na kutwaa taji lililokuwa wazi la WBC International super featherweight. Pambano hilo liliratibiwa na Supanat Chanram na Brico Santig.

Ushindi huo ulikuwa hatua muhimu kwa bondia huyo wa Tanzania, ambaye aliingia ulingoni akiwa na dhamira ya kulipiza kisasi kufuatia sare ya utata katika pambano lao la awali Februari 26, 2026.

Class alisema marudiano yalikuwa ya lazima baada ya kuwasilisha malalamiko kuhusu matokeo ya awali aliyodai hayakuwa ya haki.

“Pambano lile halikuhukumiwa kwa haki. Nililazimika kuwasilisha malalamiko kwa sababu nilijua nilifanya vizuri zaidi,” alisema.

“Marudiano haya yamenipa nafasi ya kuthibitisha uwezo wangu, na nilihakikisha hakuna shaka safari hii.”

Kuanzia raundi za mwanzo, Class alionyesha dhamira kubwa kwa kushambulia kwa nguvu na mpangilio. Baada ya kuanza taratibu, alichukua udhibiti kuanzia raundi ya pili kwa kutumia ngumi za moja kwa moja na mashambulizi ya mwili yaliyomvuruga mpinzani wake.

Katika raundi ya nne, alimwangusha mpinzani wake kwa shambulio kali. Aliendelea kutawala hadi raundi ya tano, ambapo alimwangusha tena kabla ya mwamuzi kusimamisha pambano dakika 2:59 kutokana na kipigo kikali.

Ushindi huo umeboresha rekodi yake hadi ushindi 34 (ikiwemo KO 17), kupoteza sita na sare mbili, na kumthibitisha kama mmoja wa mabondia bora nchini Tanzania.

Pamoja na mafanikio hayo, Class alisema sasa analenga mafanikio makubwa zaidi kimataifa.

“Ninajua jukumu langu lililo mbele. Ni kutetea mataji haya mawili, lakini pia kulenga mikanda mikubwa zaidi. Siwezi kurudi kwenye mapambano ya ndani kwa sababu yatapunguza hadhi yangu.

“Nahitaji kuwa makini na kuepuka mapambano yasiyo na thamani, yanayojulikana kama ‘nani mkali’. Hayo hayasaidii katika kiwango hiki,” alisema.

Class anaamini nidhamu na mipango madhubuti vitakuwa muhimu katika kukabiliana na wapinzani wakubwa zaidi.