Home Habari za michezo ROMMY3D AWATAJA BACCA, DIARRA KAMA NGUZO MUHIMU YANGA

ROMMY3D AWATAJA BACCA, DIARRA KAMA NGUZO MUHIMU YANGA

0

Baada ya dabi ya Kariakoo kati ya Simba na Yanga iliyopigwa jana Jumapili kwenye Uwanja wa Meja Jenerali Isamuhyo jijini Dar es Salaam kumalizika kwa sare ya mabao 2-2, mpiga picha maarufu nchini, Rommy3D, ameweka wazi rangi zake halisi.

Rommy amevunja ukimya na kutangaza rasmi kuwa yeye ni shabiki lialia wa klabu ya Yanga, huku akimwaga sifa kwa nyota wanaofanya kazi nzuri ndani ya kikosi hicho cha mabingwa watetezi.

Katika maelezo yake yaliyojaa mahaba kwa klabu hiyo ya Jangwani, Rommy amebainisha kuwa ubora wa Yanga kwa sasa unachagizwa na nguzo imara alizozitaja kuwa ni Ibrahim Hamad ‘Bacca’, kiungo fundi Salum Abubakar ‘Sure Boy’, pamoja na kipa stadi Djigui Diarra.

Kwa mujibu wa mpiga picha huyo, mchango wa watatu hao uwanjani umekuwa chimbuko la furaha yake kama shabiki, kutokana na kiwango chao cha hali ya juu na utulivu wanapokuwa na mpira.

Hata hivyo,  Rommy3D hakupuuza uwezo wa watani wao wa jadi Simba akisema walionyesha kiwango kizuri.

Licha ya unazi wake kwa Yanga, amekiri kuvutiwa na vipaji vya baadhi ya wachezaji wa Msimbazi, akiwataja beki mwenye mapafu ya mbwa, Shomari Kapombe, pamoja na kiungo mshambuliaji Libase Gueye.

Rommy hakusita pia kumtaja beki wa zamani wa timu hiyo, Enock Inonga, kama mmoja wa wachezaji waliomvutia zaidi licha ya kuwa tayari ameshatimka kikosini hapo.

Hatua hiyo ya Rommy3D imepokelewa kwa hisia chanya mtandaoni, ambapo wadau wengi wa soka wamesifu uwezo wake wa kutofautisha ushabiki na utaalamu wa soka.

Mashabiki wameitaja kauli yake kama ishara ya upendo na weledi, ikionyesha kuwa michezo ni chombo cha kuunganisha watu na kwamba inawezekana kabisa kuthamini kazi nzuri ya mchezaji hata kama anavaa jezi ya mpinzani wako.