Home Habari za michezo VYOMBO VIPYA TWANGA PEPETA VYAGHARIMU SH100M

VYOMBO VIPYA TWANGA PEPETA VYAGHARIMU SH100M

0

BENDI ya muziki wa dansi ya Twanga Pepeta, imepokea seti mpya ya vyombo vya muziki vilivyonunuliwa kwa ajili ya kuboresha burudani ya bendi hiyo, ambapo hadi kuwasili nchini mchakato wake umechukua takribani mwezi mmoja.

Akizungumza na Soka la Bongo, meneja wa bendi hiyo, Hassan Rehani, amesema vyombo hivyo vilivyotokea nchini China, vimegharimu zaidi ya Sh100 milioni.

Rehani ameeleza kuwa, mchakato wa ununuzi ulihusisha watu wawili waliotumwa kwenda kusimamia manunuzi hayo ili kuhakikisha wanapata vifaa vya kisasa vinavyokidhi mahitaji ya bendi hiyo.

“Vyombo hivi ni full set kwa ajili ya matumizi ya bendi. Vimechukua takribani mwezi mmoja mpaka kupokelewa rasmi jana tarehe 04 Mei 2026. Tumetumia zaidi ya milioni 100 kwa sababu tulituma watu wawili kwenda kuvichagua na kuvileta kutoka China,” amesema Hassan Rehani.

Aidha, Rehani amesema mpango uliopo sasa ni kuanza kutumia vyombo hivyo rasmi siku ya uzinduzi wa albamu mpya ya Twanga Pepeta inayotarajiwa kufanyika Agosti 7, 2026, siku ambayo itakuwa maalum kwa mashabiki wa muziki huo.

“Mpango wetu ni kuanza kuvipiga siku ya uzinduzi tarehe 7 Agosti 2026. Hiyo ndiyo siku ambayo mashabiki wataanza kusikia ladha mpya ya Twanga Pepeta na vyombo hivi vipya,” ameongeza.

Meneja huyo ameweka wazi pia kuwa kabla ya uzinduzi mkuu, kutakuwa na uzinduzi mdogo wa kuvitambulisha vyombo hivyo kwa mashabiki na wadau wa muziki, ili kuwapa nafasi ya kuviona na kuvisikia kabla ya tukio kubwa.

“Vyombo vitazinduliwa kabla ya uzinduzi wa albamu. Tunataka mashabiki wetu wapate nafasi ya kuviona na kuvisikia mapema kabla ya siku ya tukio kuu,” amesisitiza Rehani.