“Wanakula majasho yetu, wanakula mikamasi yetu, kocha anakwambia ‘jabu’ ukipiga jasho limemdondokea mdomoni, lakini hakuna wanachopata kutokana na pesa ambayo tunalipwa kwenye mapambano, makocha wanastahili kupewa kipaumbele sana,” anasema.
SABABU YA KUFUNGIWA
Mwenga amefungiwa mwaka mmoja hadi Machi 28, 2027, kufuatia kugoma kushuka ulingoni akipinga matokeo ya pambano alilodai kuonewa.
Hiyo ilikuwa Machi 26, 2026 jijini Dar es Salaam alipopanda ulingoni kupambana na Wazir Magombana na kupoteza kwa pointi.
Katika pambano hilo, kwa mujibu wa Boxrec, majaji wote watatu walimpa ushindi Magomba ambapo wote walitoa alama 60, huku wakimpa Mwenga 54.
Bondia huyo anaomba radhi kwa Kamisheni ya Ngumi za kulipwa Tanzania (TPBRC) na Baraza la Michezo la Taifa (BMT) kutokana na kitendo alichokifanya.
“Naomba wanifungulie ili niweze kupigana, inanikwamisha kwenye ndoto zangu,” anasema.
SOKA
Kabla ya ngumi, Mwenga alikuwa akicheza mpira wa miguu nafasi ya beki wa kulia akishiriki Ligi Daraja la Tatu akiwa na timu ya FC Tabora. Mwaka 2010 alifanikiwa kushiriki mashindano ya UMISETA. Lakini baadaye aliamua kuacha mpira wa miguu kwa sababu aliona kuna watu wenye uwezo mkubwa zaidi yake, akaamua kuelekeza nguvu zake kwenye ndondi.
Anasema yeye ni shabiki mkubwa wa Yanga kwa Tanzania na nje ni Manchester United.
MALENGO YAKE
Bondia huyo anasema ana malengo makubwa ya kushinda mikanda ya WBC na WBO na kuwa bondia anayetajwa duniani kama Floyd Mayweather, Mike Tyson, au Gervonta Davis.
Anaamini akifunguliwa, ndani ya kipindi cha miaka miwili atafikia kiwango hicho cha dunia na kutimiza malengo yake ambayo kwa watu wanaweza wasiamini ila kwake inawezekana.
“Mimi nina malengo makubwa na nilijiwekea mapema lakini adhabu imeniharibia, naamini kwa uwezo wangu nitafikia kile ninachokikusudia kwa sababu nina kiwango,” anasema Mwenga ambaye nje ya ngumi ana ujuzi wa ufundi wa magari, fani aliyoisomea kabla hata hajaingia kwenye mchezo huo.