Habari za michezo

SINGIDA BS YAKOLEZA VITA TOP FOUR IKIINYUKA MTIBWA

Vardo May 9, 2026 10:35 pm

USHINDI mnono wa mabao 4-0 walioupata Singida Black Stars dhidi ya Mtibwa Sugar, umeongeza presha kwenye vita ya nne bora ya Ligi Kuu Bara huku timu hiyo ikiendelea kujiweka pazuri kuelekea mwisho wa msimu.

Mechi hiyo iliyopigwa leo Mei 9, 2026 kwenye Uwanja wa Airtel uliopo Singida, ulikuwa na kasi kubwa, Singida ilionyesha ubora kuanzia dakika za mwanzo na kufanikiwa kupata bao la kuongoza kupitia kwa Mosi Nduwumwe dakika ya 10 kabla ya mshambuliaji huyo kuongeza la pili dakika ya 42 na kuifanya timu hiyo kwenda mapumziko ikiwa mbele kwa mabao 2-0.

Kipindi cha pili wenyeji waliendelea kutawala mchezo huku Lamine Jarjou akiifungia timu hiyo bao la tatu dakika ya 52 kabla ya Emmanuel Keyekeh kuhitimisha karamu ya mabao dakika ya 68.

Matokeo hayo yameifanya Singida Black Stars kufikisha pointi 35 baada ya kucheza mechi 22 na kusogea nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi, hatua inayoongeza ushindani mkubwa katika eneo la timu zinazowania nafasi za juu msimu huu.

Licha ya kupanda nafasi ya nne, Singida bado inaendelea kuviziana kwa karibu na TRA United ambayo ipo nafasi ya tano ikiwa na pointi 33 baada ya kucheza idadi sawa ya mechi. Tofauti ya pointi mbili pekee inaifanya vita hiyo kuwa wazi huku kila timu ikisaka nafasi ya kumaliza juu.Kwa upande mwingine, ushindi huo unaifanya Singida kuendelea kuisogelea Azam FC iliyopo nafasi ya tatu na pointi 43, huku vigogo Yanga na Simba wakiendelea kung’ang’ania nafasi hizo mbili za juu.

MKUDE AWAINGIZA WANAJESHI VITANI TRA UNITED YAVUNJA REKODI NNE ZA AZAM FC