Habari za michezo
NICOLAS JACKSON ANUKIA KUTUA ITALIA, JUVENTUS YATAJWA
JUVENTUS inatajwa kufikiria kutuma ofa ya kumsajili kwa mkopo kwa mshambuliaji wa Chelsea, Nicolas Jackson, katika dirisha lijalo la usajili wa majira ya kiangazi.
Nyota huyo wa kimataifa wa Senegal mwenye umri wa miaka 24 kwa sasa anaitumikia Bayern Munich kwa mkopo, lakini taarifa zinaeleza kuwa hatobaki ndani ya kikosi hicho cha mabingwa wa Bundesliga msimu ujao kwani hawajaridhishwa na kiwango chake.
Juventus inaonekana kutafuta kuongeza nguvu kwenye safu yao ya ushambuliaji baada ya kutofanya vizuri msimu huu kuanzia michuano ya ndani na kimataifa.
Nicolas mwenyewe amewaambia wawakilishi wake kwamba haitaji tena kuichezea Chelsea, hivyo kwa msimu ujao ni aidha auzwe ama atolewe kwa mkopo wa msimu mmoja.
Mkataba wa sasa wa Jackson na Chelsean unatarajiwa kumalizika mwaka 2033 na akiwa na Bayern msimu huu amecheza mechi 33 za michuano yote na kufunga mabao 10.
Chelsea pia haionekani kuwa na mpango wa kuendelea kuwa naye, hivyo ikiwasilishwa ofa kutoka kwa timu inayomhitaji itakuwa tayari kumuuza.
Jarrod Bowen
MSHAMBULIAJI wa West Ham, Jarrod Bowen ameibuka kwenye rada za vigogo wa Ligi Kuu England, Liverpool, Newcastle United na Everton dirisha lijalo la usajili.
Bowen, 29, amekuwa akifuatiliwa kwa karibu na vigogo hao kutokana na kiwango chake bora akiwa na West Ham United, huku taarifa zikieleza klabu hizo zitaendelea kuwania saini yake hata kama West Ham itaepuka na janga la kushuka daraja mwishoni mwa msimu huu.
Dani Ceballos
REAL Madrid inaweza kulazimika kuuza baadhi ya wachezaji wake kabla ya kufanya usajili mpya dirisha lijalo la majira ya kiangazi.
Kiungo wa kimataifa wa Hispania, Dani Ceballos, 29, ni miongoni mwa wachezaji wanaoweza kuondolewa ikiwa mabosi wa Madrid wataamua kupunguza mastaa ili kutengeneza nafasi ya usajili mpya.
Ceballos amekuwa akihusishwa mara kadhaa kuondoka kwa sababu hapati nafasi ya kutosha katika kikosi cha kwanza.