Habari za michezo

FOUNTAIN GATE YAIBANIA JKT TANZANIA

Vardo May 21, 2026 10:52 pm

FOUNTAIN Gate imewazuia JKT Tanzania kukaa nafasi ya nne kwenye msimamo wa Ligi Kuu ya NBC baada ya kuwalazimisha sare ya mabao 2-2 kwenye mchezo uliopigwa katika Uwanja wa Meja Isamuhyo, Mbweni.

Huu ulikuwa mchezo wa Ligi Kuu ambao ulikuwa unasubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wa soka kwa kuwa kama JKT ingepata ushindi ingefanikiwa kukaa nafasi ya nne kwenye msimamo wa ligi na kuwashusha Singida BS.

Matokeo haya yameendelea kuwa bora kwa Fountain baada ya sasa kufikisha pointi 26 na kukaa katika nafasi ya 11 kwenye msimamo ikiwa tofauti ya pointi tisa dhidi ya timu inayoweza kushuka daraja mwisho wa msimu baada ya kucheza michezo 23.

Kwa upande wa JKT yenyewe imefikisha pointi 37 ikiwa nafasi ya sita baada ya kucheza michezo 23, ikiwa ni moja zaidi ya zile ambazo ilimaliza nazo msimu uliopita ambapo ilikuwa na pointi 36 kwenye michezo 30, kama ingeshinda ingekuwa na pointi 39 na kukwea hadi nafasi ya nne.

Fountain ambayo inafundishwa na kocha Fred Felix Kataraiya ‘Minziro’ ndiyo ilikuwa ya kwanza kujipatia mabao yake kupitia kwa Juma Abushiri katika dakika ya tatu,  Ismail Aziz Kader dakika 45.Kipindi cha pili, JKT ilicharuka na kurudisha mabao hayo kupitia kwa Saleh Karabaka katika dakika 54 ya mchezo huku Paul Peter, akifunga moja kati ya mabao bora kwenye ligi msimu huu katika dakika 86 na kuifanya mechi hiyo kumalizika kwa sare hiyo ambayo ni ya kumi kwa JKT na tano kwa Fountain Gate hadi sasa.

SIMBA WAUA MZUKA WA COASTAL, YANGA ATELEZA KWENYE KILELE CLARA LUVANGA ANG’ARA TENA SAUDIA