Habari za michezo

KAGERA SUGAR, GEITA GOLD KATIKA VITA YA KILELENI CHAMPIONSHIP

Vardo May 23, 2026 9:57 am

LEO utashuhudiwa utamu wa Ligi ya Championship ukiendelea katika viwanja mbalimbali, ila moja ya mechi inayosubiriwa kwa hamu kubwa na mashabiki wengi ni ya vinara Geita Gold itakayokuwa ugenini dhidi ya Kagera Sugar.

Mechi hiyo itakayopigwa Uwanja wa Kaitaba, Bukoba, inavuta hisia za mashabiki wa soka kutokana na nafasi za timu hizo mbili na gepu la pointi ilizopishana na huenda ikatoa taswira ya atakayekuwa bingwa wa Championship msimu huu.

Geita Gold inaongoza na pointi 64, ikishinda mechi 20, sare nne na kupoteza moja, huku Kagera inayoshika nafasi ya pili na pointi 61, ikiwa imeshinda 19, sare nne na kupoteza mbili kati ya 25 ambazo timu zote mbili zimecheza hadi sasa.

Timu zote mbili zinaingia katika mechi hiyo zikiwa na matokeo mazuri ya mwisho na Kagera ikiwa nyumbani iliifunga Mbuni FC ya Arusha mabao 2-0, huku kwa upande wa Geita Gold ikitoka kuichapa TMA FC ya Arusha mabao 4-0.

Mechi ya raundi ya kwanza ya timu hizo iliyopigwa Uwanja wa Nyankumbu, mjini, Geita, Desemba 21, 2025, Geita Gold ilishindwa kutamba nyumbani na kulazimishwa sare ya bao 1-1, jambo linalosubiriwa kuona leo itakuwaje ikicheza ugenini.

Mara ya mwisho kwa timu hizo kukutana kwenye Uwanja wa Kaitaba, ilikuwa mechi ya Ligi Kuu msimu wa 2023-2024, Septemba 17, 2023, na Kagera Sugar ilishinda bao 1-0, la aliyekuwa beki wa timu hiyo, Mganda Dissan Galiwango dakika ya 90+4.

Katika mechi ya raundi ya pili ya Ligi Kuu msimu wa 2023-2024, zilipokutana Februari 28, 2024 kwenye Uwanja wa Nyankumbu mjini, Geita, wenyeji Geita Gold ilitoka suluhu (0-0), huku ukiwa ni msimu wa mwisho kwa kikosi hicho kucheza Ligi Kuu.

Kagera iliyodumu katika Ligi Kuu Bara kwa miaka 20 tangu ilipoanza kushiriki 2005, ilishuka daraja msimu wa 2024-2025, baada ya kushinda mechi tano, sare nane na kupoteza 17, ikimaliza ikiwa nafasi ya 15 na pointi 23.

Timu hiyo inayonolewa na aliyekuwa nyota wa Simba, Yanga na timu ya Taifa Stars, Juma Kaseja aliyewahi kuitumikia pia Kagera akiwa mchezaji na kocha wa makipa, ana kazi ya kukipambania kikosi hicho ili kirejee tena katika Ligi Kuu Bara.

Kwa upande wa Geita iliyoshuka daraja msimu wa 2023-2024, msimu wa 2024-2025, wa Championship ilimaliza nafasi ya nne na pointi 56, ikiwa na aliyekuwa Kocha, Mohamed Muya na kushindwa kurejea Ligi Kuu, baada ya kufeli mechi za ‘Play-Off’.

Geita ilicheza ‘Play-Off’ ya kupanda Ligi Kuu Bara dhidi ya Stand United, ‘Chama la Wana’ iliyomaliza nafasi ya tatu na pointi 61 na kushuhudiwa ikiondoshwa kwa jumla ya mabao 4-2, baada ya sare nyumbani ya 2-2, kisha kuchapwa ugenini 2-0.

Timu hiyo inayofundishwa na Kocha, Zubery Katwila aliyejiunga nayo akitokea Bigman FC, anaipambania kuirejesha Ligi Kuu Bara kutokana na uzoefu wake mkubwa wa kuzifundisha pia, Ihefu ambayo kwa sasa ni Singida Black Stars na Mtibwa Sugar.

Mechi nyingine za leo itashuhudiwa Hausung FC iliyotoka kuchapwa mabao 3-0, ugenini dhidi ya Bigman FC ikirejea kwenye Uwanja wa Amani uliopo mjini Njombe kwa kuikaribisha B19 FC, yenye kumbukumbu nzuri baada ya kuichapa Mbeya Kwanza 1-0.

KenGold baada ya kuchapwa mabao 3-1, dhidi ya Polisi Tanzania mechi ya mwisho, inarejea kwenye Uwanja wa Halmashauri ya Chunya jijini, Mbeya kuikaribisha Songea United, iliyotoka pia kupoteza Tanga kwa kufungwa na African Sports mabao 3-0.

Kwenye Uwanja wa Sheikh, Amri, Abeid, jijini, Arusha kutakuwa na ‘Derby ya Monduli’, ambapo Mbuni FC iliyotoka kuchapwa mabao 2-0, dhidi ya Kagera Sugar itapambana na majirani zao wa TMA FC, iliyochapwa pia na Geita Gold ugenini mabao 4-0.  Baada ya Mbeya Kwanza kushangazwa na B19 FC kwa kuchapwa bao 1-0, mechi iliyopita jijini, Dar es Salaam, inarudi kwenye Uwanja wa Ali Hassan Mwinyi, mjini, Tabora kwa kuikaribisha Bigman FC ya Lindi, iliyotoka kuichapa Hausung FC mabao 3-0.

Kwenye Uwanja wa Mkwakwani Tanga, African Sports baada ya kuichapa Songea United mabao 3-0, itaikaribisha maafande wa Polisi Tanzania iliyoichapa KenGold ya Mbeya 3-1, huku Barberian ikicheza dhidi ya kikosi cha maafande wa Transit Camp.

Barberian iliyotoka sare ya bao 1-1, dhidi ya Stand United, itakuwa kwenye Uwanja wa Filbert Bayi mkoani Pwani kucheza na maafande wa Transit Camp yenye kumbukumbu mbaya baada ya kikosi hicho kuchapwa na Gunners FC kutoka Dodoma mabao 3-1.

Raundi ya 26 itahitimishwa kesho Jumapili kwa mechi moja kupigwa kwenye Uwanja wa Jamhuri jijini, Dodoma na Gunners iliyoichapa maafande wa Transit Camp mabao 3-1, itaikaribisha Stand United iliyotoka sare ya 1-1, dhidi ya Barberian FC.

Stand United ‘Chama la Wana’, ilishuka daraja msimu wa 2018-2019, ikimaliza nafasi ya 19 na pointi 44 baada ya timu hiyo yenye maskani yake huko Shinyanga kushinda mechi 12, ikitoka sare nane na kupoteza 18, ikifunga mabao 38 na kuruhusu 50.

Msimu uliopita, Stand ilimaliza ikiwa nafasi ya tatu na pointi 61, ambapo ilicheza ‘Play-Off’ ya kupanda Ligi Kuu Bara, ikianza kwa kuiondosha Geita Gold iliyomaliza ya nne na pointi 56, katika Ligi ya Championship kwa jumla ya mabao 4-2.

Baada ya Stand kuitoa Geita Gold, ikacheza ‘Play-Off’ nyingine na Fountain Gate iliyotolewa pia hatua hiyo na maafande wa Tanzania Prisons kwa jumla ya mabao 4-2, ambapo kikosi hicho kilikwama kupanda baada ya kufungwa jumla ya mabao 5-1.

Kwa upande wa Fountain, ilimaliza nafasi ya 14 na pointi 29 katika Ligi Kuu msimu wa 2024-2025 na kukutana na Tanzania Prisons iliyomaliza ya 13 na pointi 31, kwenye mechi ya mtoano na kikosi hicho cha maafande kushinda jumla ya mabao 4-2.

BONUS ZA CAF ZATUA LIGI KUU KWA MASTAA WA YANGA WPL KUNA MECHI MBILI ZA UAMUZI