DAKIKA 1,080 MTIBWA SUGAR BILA USHINDI UGENINI
MTIBWA Sugar imeendeleza rekodi ya kutopata ushindi katika mechi za Ligi Kuu Bara ugenini, baada ya leo kukubali kipigo cha bao 1-0 dhidi ya Mbeya City ukiwa ni mchezo wa 12 bila kuonja pointi tatu.
Mchezaji Adil Buha ndiye aliyeibuka shujaa katika mchezo huo kufuatia bao lake la dakika ya 36 kwa mkwaju wa penalti lililoihakikishia pointi tatu Mbeya City na kuendeleza matumaini ya kukwepa kushuka daraja.
Hata hivyo, licha ya ushindi huo, timu hiyo inayomilikiwa na Halmashauri ya Jiji la Mbeya imebaki katika nafasi ya 14 kwa pointi 25 ikibakiza mechi nne kumaliza msimu na kusubiri hatma yake.
Baada ya mchezo huo, City itabaki nyumbani Uwanja wa Sokoine kuwasubiri Simba, mchezo utakaopigwa Juni 17, saa 8 mchana, ikihitaji ushindi ili kujinasua nafasi za chini na kuongeza matumaini ya kukwepa kushuka daraja.
Katika mchezo wa leo timu zote zilionyesha ubora na uwezo binafsi, lakini wenyeji ndio walifaidika na dakika 90 kutokana na ushindi ambao umewaamsha upya katika kampeni ya kubaki Ligi Kuu.
Licha ya kupoteza mchezo huo, lakini Mtibwa Sugar hawakuwa wanyonge kutokana na kumiliki mpira kwa asilimia kubwa japokuwa watajilaumu kwa nafasi walizopata bila kuzitumia.
Timu hiyo iliyorejea Ligi Kuu msimu huu imefikisha mechi 12 ugenini bila kuonja ushindi ikiwa imepoteza mechi saba na kutoa sare michezo mitano na kuwa nafasi ya 11 kwa pointi 27 ikibakiza nne kuhitimisha msimu huu.
Akizungumzia matokeo hayo, Kocha mkuu wa timu hiyo, Yusuph Chipo, amesema huenda haikuwa bahati kwao kwa kuwa nyota wake walioneysha kiwango bora, lakini wakakosa kutumia nafasi walizopata kufunga mabao.
“Tunakwenda kujipanga upya na tuwapongeze wapinzani waliopata bahati kushinda. Tunazo mechi nne za kupambania kubaki salama Ligi Kuu. Vita ni ngumu, lakini tunao uwezo wa kufanya tunachotarajia,” amesema Chipo.
Kocha Msaidizi wa Mbeya City, Patrick Mwangata amewapongeza wachezaji kwa kujituma na kufanikisha ushindi akieleza kuwa matokeo hayo yameongeza kitu katika kukwepa kushuka daraja.
“Tunakwenda kujipanga upya na mchezo ujao dhidi ya Simba. Tunajua ugumu na umuhimu wake. Tutawaandaa vyema wachezaji kiakili na kisaikolojia kuhakikisha tunapata pointi tatu tuweze kujinasua mkiani,” amesema kocha huyo.