UKWELI MCHUNGU…HIVI NDIVYO YANGA WANAVYOANZA KUPOTEANA MAZIMA…..
HATIMAYE Yanga imekuwa na siku 39 za majanga baada ya kushuhudiwa ikitema rasmi ubingwa wa Kombe la CRDB ambao iliuchukua kwa misimu minne mfululizo, kufuatia kuchapwa mabao 3-2, na Azam FC kwenye Uwanja CCM Kirumba, Mwanza.
Msimu uliopita wakati kama huu tayari ilikuwa imetwaa Kombe la Mapinduzi na Muungano na wamefuzu kwa fainali ya Kombe la CRDB.
Msimu huu tayari wamepoteza Kombe la Muungano kwa Simba na sasa wametolewa katika nusu fainali ya Kombe la Shirikisho.
Siku hizo 39, zimeanza tangu ilipochapwa mabao 3-2, dhidi ya Dodoma Jiji, Mei 13, 2026, katika mechi ya Ligi Kuu, ikiwa ni kichapo cha kwanza pia, tangu mara ya mwisho ilipofungwa na Tabora United sasa TRA United mabao 2-1, Novemba 7, 2024.
Mwanzo wa Anguko: Kipigo cha Dodoma Jiji Kilitibua Rekodi ya Siku 552
Ushindi wa mabao 3-2, ilioupata Dodoma Jiji katika mechi ya Ligi Kuu Bara dhidi ya Yanga, Mei 13, 2026, ulivunja rasmi rekodi ya mabingwa hao watetezi ya kucheza muda mrefu bila ya kupoteza, tangu mara ya mwisho ilipokuwa Novemba 7, 2024.
Dodoma Jiji ilivunja rasmi rekodi hiyo ya Yanga ya kucheza mechi 42 za Ligi Kuu Bara bila kupoteza tangu mara ya mwisho ilipochapwa na Tabora United sasa TRA United mabao 3-1, mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Azam Complex, Novemba 7, 2024.
Kabla ya kichapo hicho, Yanga ilicheza mechi 42 za Ligi Kuu Bara bila ya kupoteza kwa siku 552, ambazo ni sawa na mwaka mmoja, miezi sita na siku sita, rekodi ambayo ilivunjwa na Dodoma Jiji wakati timu hiyo ilipochapwa 3-2, Mei 13, 2026.
Mbali na Dodoma Jiji kuvunja rekodi hiyo ya Yanga, ila timu hiyo iliandika historia mpya ya kushinda kwa mara ya kwanza dhidi ya kikosi hicho, kwani tangu kilipopanda Ligi Kuu msimu wa 2020-2021, ilikuwa haijawahi kushinda hata mechi moja.
Tangu Dodoma Jiji ianze kucheza Ligi Kuu Bara msimu wa 2020-2021, ushindi huo wa mabao 3-2, Mei 13, 2026, ulikuwa ni wa kwanza katika historia yake dhidi ya Yanga, kwani kabla ya hapo ilicheza jumla ya mechi 11, ikichapwa 10 na sare moja.
Baada ya hapo jinamizi likaendelea kuikumba timu hiyo baada ya kuchapwa mabao 3-2, dhidi ya Azam FC katika Kombe la CRDB Juni 21, 2026 na kutimiza siku 39, tangu ilipofungwa pia 3-2 na Dodoma Jiji kwenye Uwanja wa Liti, Singida Mei 13, 2026.
Katika mechi hiyo ya kichapo cha mabao 3-2, ilichokipata Yanga dhidi ya Azam FC kwenye hatua ya nusu fainali ya Kombe la CRDB iliyopigwa kwenye Uwanja wa CCM Kirumba, Mwanza, kikaivunja tena rekodi ya kikosi hicho iliyodumu kwa muda mrefu.
Timu hizo zilikutana Juni 21, 2026, tangu mara ya mwisho zilipokutana Aprili 25, 2026, katika mechi ya nusu fainali ya Kombe la Muungano iliyopigwa kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, visiwani Zanzibar na Yanga kuibuka na ushindi wa 2-1.
Bao la Azam lilifungwa na Feisal Salum ‘Fei Toto’ huku ya Yanga yakifungwa na Prince Dube na Maxi Nzengeli na kuipeleka fainali timu hiyo na kushuhudiwa ikishindwa kutamba baada ya kuchapwa 1-0, dhidi ya watani zao Simba, Aprili 29, 2026. Baada ya siku 57, tangu mara ya mwisho Azam FC na Yanga zilipokutana visiwani Zanzibar, hatimaye miamba hiyo ikakutana tena Juni 21, 2026, ila ikiwa ni nusu fainali ya Kombe la CRDB na matajiri hao wa Jiji la Dar es Salaam wakashinda 3-2.
Yanga ambao ni mabingwa wa Kombe la CRDB kwa misimu minne mfululizo, iliingia katika mechi hiyo ikiwa na rekodi nzuri tofauti na wapinzani wao Azam, kwani kikosi hicho kilikuwa hakijapoteza kwenye mashindano hayo tangu, Julai 25, 2021.
Tangu Julai 25, 2021, Yanga ilipochapwa na Simba bao 1-0, katika mechi ya fainali ya Kombe la CRDB kwenye Uwanja wa Lake Tanganyika Kigoma, timu hiyo ilikuwa haijapoteza ikitimiza siku 1,792, ambazo Azam FC imezivunja rasmi kwa kikosi hicho.
Katika mechi hiyo ya Julai 25, 2021, Simba ilishinda bao 1-0, lililofungwa na Mganda Taddeo Lwanga dakika ya 80, ambapo tangu hapo Yanga imetimiza miaka mitano, miezi 10 na siku 27 bila kupoteza, rekodi ambayo tayari Azam imeivunja rasmi. Tangu mechi ya fainali ya Julai 25, 2021, Yanga ilicheza jumla ya mechi 28 za Kombe la CRDB na kushinda yote kabla ya kutibuliwa rekodi yake na Azam, huku kati ya hiyo safu ya ushambuliaji ya kikosi hicho ilifunga mabao 84 na kuruhusu 10.
Kabla ya hapo, Azam FC ilikutana na Yanga mara mbili katika Kombe la CRDB na kuchapwa mechi zote za fainali, ikianza na bao 1-0, lililofungwa na Mzambia Kennedy Musonda mechi iliyopigwa kwenye Uwanja wa Mkwakwani mjini Tanga, Juni 12, 2023.
Timu hizo zikakutana tena hatua ya fainali ya Kombe la CRDB msimu wa 2023-2024, ambapo Yanga ilishinda kwa penalti 6-5, baada ya suluhu (0-0) ya dakika 120, kwenye Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar, Juni 2, 2024. Kwa maana hiyo, Azam FC imeandika rekodi mpya ya kushinda mechi ya kwanza ya Kombe la CRDB dhidi ya Yanga tangu msimu wa 2015-2016, huku ikivunja pia historia ya kucheza kwa muda mrefu bila kupoteza ikitumia siku 1,792, tangu Julai 25, 2021.
SAFARI ILIVYOKUWA
Katika michuano ya CRDB msimu huu, Yanga ilianza kutetea taji hilo kwa kuichapa Cosmopolitan mabao 2-0, huku Azam FC ikiifunga Endument FC kutoka Kilimanjaro bao 1-0.
Raundi ya 32, Yanga ikakutana na Polisi Tanzania na kukitembezea kichapo cha mabao 7-1, huku Azam FC ikiifunga Mbeya Kwanza bao 1-0.
Safari ya matumaini ikaendelea kwa timu hizo na hatua ya 16 bora Yanga ikakutana na TMA FC inayoshiriki Championship na kuichapa bao 1-0, huku wapinzani wake pia Azam FC ilicheza na Fountain Gate na kuibuka na ushindi mabao 4-0. Katika hatua ya robo fainali, Yanga ikakutana na JKT Tanzania na kikosi hicho kikashinda mabao 2-0, huku Azam ikaichapa Mashujaa bao 1-0 na timu hizo kukata tiketi ya kucheza nusu fainali iliyokuwa mwisho wa safari ya Yanga.