Lionel Messi, Kylian Mbappe Kama Pacha
BOSTON, MAREKANI: KYLIAN Mbappe ameiongoza Ufaransa kutinga hatua ya nusu fainali ya Kombe la Dunia baada ya kufunga bao katika ushindi wa mabao 2-0 dhidi ya Morocco, akijibu kwa vitendo baada ya kukosa penalti mapema katika mchezo huo.
Kombe hili la Dunia limekuwa la kipekee si kwa ubora wa timu pekee, bali kwa vita ya mastaa hawa wawili wanaobadilishana makofi ya kisoka kila hatua ya mashindano na ni dhahiri kuwa mwishoni mmoja wao anapewa nafasi kubwa ya kuwa mchezaji bora wa michuano hii.
Mbappe alianza kwa kufunga mabao mawili dhidi ya Senegal katika mchezo wa ufunguzi wa Ufaransa, kabla Messi hajibu kwa hat-trick dhidi ya Jordan siku iliyofuata. Kadiri mashindano yalivyoendelea, kila mmoja amekuwa akijibu alichofanya mwenzake, jambo lililoongeza msisimko mkubwa kuelekea hatua za mwisho.
Dhidi ya Morocco, Mbappe alipata wakati mgumu baada ya penalti yake kuokolewa na kipa Yassine Bounou, lakini hakukata tamaa. Alirejea kipindi cha pili na kufunga bao muhimu lililoivusha Ufaransa kwenda nusu fainali.
Kilichovutia zaidi ni kwamba tukio hilo lilifanana na alichokifanya Messi katika mchezo wake dhidi Misri, ambapo pia alikosa penalti kabla ya kufunga bao muhimu lililoiwezesha Argentina kusonga mbele.
Sasa macho yote yanaelekezwa kwenye pambano la wawili hao, huku kila mmoja akisaka kumaliza mashindano akiwa kinara wa mabao na pia kubeba taji la dunia.
Miaka minne iliyopita, Mbappe alifunga ‘hat-trick’ kwenye fainali lakini Messi ndiye aliyeinua Kombe la Dunia. Safari hii, ushindani wao unaonekana kuwa mkubwa zaidi, hasa ikizingatiwa kuwa hii ndiyo Kombe la Dunia la mwisho kwa Messi, huku Mbappe akitajwa kuwa mrithi wake kwenye soka la dunia.
Wakati huohuo, nguli wa zamani wa Manchester United, Roy Keane, amemsifu Mbappe kwa kiwango alichoonyesha dhidi ya Morocco, akisema mshambuliaji huyo ndiye anayekuwa na udhibiti wa kila hali anapokuwa uwanjani.
“Wachezaji wakubwa huamua wanachotaka kufanya. Mabeki wanamuogopa kwa sababu anaweza kuwazunguka au kukimbia nyuma yao, hivyo hawajui wafanye nini. Mbappe ndiye anayeongoza kila hali anayokutana nayo uwanjani,” alisema Keane.
Keane pia alimtetea Mbappe baada ya kukosa penalti, akieleza kuwa kusubiri kwa zaidi ya dakika tatu kabla ya kuipiga penalti hiyo kulimuongezea presha isiyo ya kawaida.
“Si haki kwa mshambuliaji kusubiri zaidi ya dakika tatu kupiga penalti. Muda ni adui wa mshambuliaji na unampa faida kipa. Hata kwa mchezaji wa kiwango cha dunia, hali hiyo si rahisi,” aliongeza Keane.
Sasa swali kubwa linalobaki ni nani atatoa pigo la mwisho kati ya Mbappe na Messi katika mbio za kutwaa Kombe la Dunia na kuandika historia nyingine kubwa ya soka duniani.’’