AFCON 2027: Zanzibar Yajipanga Kivingine, Miundombinu Na Fursa Za Kiuchumi Kuruha
SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar (SMZ) inaendelea kuongeza kasi katika maandalizi ya Fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika (AFCON 2027) kwa kuboresha sekta muhimu za miundombinu ya michezo, afya na usafiri.
Akizungumza kuhusu maandalizi hayo, Kamishna wa Idara ya Mipango na Maendeleo ya Kisekta kutoka Tume ya Mipango Zanzibar, Mohamed Massoud Salim, alibainisha kuwa lengo kuu la Serikali ni kuhakikisha michuano hiyo inaleta tija katika kukuza uchumi, kuongeza nafasi za ajira na kuimarisha huduma za kijamii.
“Zanzibar kuwa mwenyeji wa AFCON inatoa fursa kubwa ya kuongeza shughuli za kiuchumi, hususani katika sekta ya utalii, usafiri na biashara ndogondogo,” alisema Salim.
Serikali pia inaangalia namna bora ya kuwashirikisha wananchi kikamilifu pamoja na sekta binafsi ili kuimarisha huduma zitakazokidhi viwango vya kimataifa wakati wa kuwapokea wageni wengi wanaotarajiwa.
Michuano ya AFCON 2027 itatimua vumbi kuanzia Juni 19 hadi Julai 17, 2027, ikiratibiwa kwa pamoja na nchi za Tanzania, Kenya na Uganda. Kwa mujibu wa Shirikisho la Mpira wa Miguu Afrika (CAF), mechi zitakazopangwa nchini Tanzania zitafanyika katika viwanja vya Dar es Salaam, Arusha na Zanzibar.