Lisa Baum Aanza Na Bao Arsenal Dhidi Ya Brighton WSL
LONDON, ENGLAND: Mshambuliaji mwenye asili ya Tanzania, Lisa Baum, ameanza maisha yake ndani ya Arsenal ya Wanawake kwa kishindo baada ya kufunga bao katika mchezo wake wa kwanza kabisa wa Ligi Kuu ya Wanawake England (WSL) dhidi ya Brighton uliochezwa uwanja wa Broadfield, leo Jumapili Septemba 6, 2026.
Baum (19) alihitaji dakika 10 pekee kufungua akaunti yake ya mabao klabuni hapo. Nyota huyo alipenya katikati ya mabeki wa Brighton na kuachia shuti kali lililopiga mwamba wa juu kabla ya kutumbukia nyavuni.
Mchezaji huyo amejiunga na Arsenal katika dirisha hili la usajili la majira ya kiangazi akitokea RB Leipzig ya Ujerumani. Katika mechi hiyo, alianza kikosini pamoja na wachezaji wengine wapya kama kipa Misa Rodriguez, beki Ona Batlle, na kiungo Georgia Stanway.
Arsenal ilipata nafasi ya kuongeza bao muda mfupi baadaye kupitia kwa Alessia Russo, lakini alipiga mpira juu ya lango lililokuwa wazi.
Brighton pia ilijaribu kurudi mchezoni ambapo Kiko Seike aliona shuti lake likiokolewa na Rodriguez, huku Fran Kirby akipiga mpira nje ukiwa karibu na lango. Beki Charlie Rule naye alijaribu shuti la mbali lililokosa shabaha.
Katika kipindi cha pili, Stina Blackstenius alikaribia kufunga bao la pili la Arsenal, lakini kipa wa Brighton, Chiamaka Nnadozie, alifanya kazi ya ziada na kucheza mpira huo uliokuwa ukielekea kona ya chini.
Ushindi huo unaifanya Brighton kupoteza mchezo wake wa kwanza wa msimu kwa mara ya pili pekee katika kipindi cha misimu nane iliyopita ya WSL.
Uraia Na Historia Ya Lisa Baum
Baum, ambaye aliichezea timu ya taifa ya Ujerumani ya vijana (U-20) kwenye Kombe la Dunia 2022, alizaliwa mwaka 2006 jijini Dar es Salaam. Mama yake ni Mtanzania na baba yake ni Mjerumani. Mwenyewe amewahi kunukuliwa akibainisha kuwa hajakata tamaa ya kuichezea timu ya taifa ya wanawake ya Tanzania, Twiga Stars.
Kijana huyo alianza safari yake ya soka katika klabu za MTV Ahrensbök na TSV Pansdorf kabla ya kujiunga na akademi ya Hamburger SV (HSV) mwaka 2021. Akiwa HSV, alisaidia timu ya vijana kutwaa ubingwa wa Ujerumani na baadaye akapandishwa kikosi cha wakubwa kilichopanda daraja hadi 2. Bundesliga na hatimaye Bundesliga.
Mwaka 2025, alijiunga na RB Leipzig ambako alicheza mechi 25 za Bundesliga na kufunga mabao sita kabla ya kunaswa na miamba ya soka England, Arsenal.