Home Yanga SC JOB: SIJAJA YANGA KUKAA BENCHI

JOB: SIJAJA YANGA KUKAA BENCHI


KITASA mpya wa klabu ya Yanga, Dickson Job amefunguka kuwa amejiunga na klabu hiyo akijua wazi atakutana na ushindani mkubwa wa namba lakini amejipanga kupambana kupata nafasi ndani ya kikosi cha kwanza.

Job alikamilisha usajili wa kujiunga na Yanga katika dirisha dogo la usajili na kukifanya kikosi hicho kufikisha idadi ya mabeki watano wa kati, eneo ambalo limekuwa likitawaliwa na Manahodha Lamine Moro na Bakari Mwamnyeto.

Job tayari amekwishaanza kujifua na kikosi cha Yanga kilichopiga kambi huko Avic Town Kigamboni jijini Dar es Salam tangu Januari 25.

Akizungumzia nafasi yake ndani ya kikosi cha Yanga, Job amesema: “Wakati nafikia maamuzi ya kujiunga na Yanga, nilijua wazi kuwa naenda kwenye timu ambayo ina ushindani mkubwa wa namba hasa katika eneo ninalotumikia kutokana na uwepo wa wachezaji wengi bora wanaocheza katika eneo hilo.

“Lakini kama mchezaji mwenye ndoto kubwa lazima ukubali changamoto kubwa hivyo naamini nitapambana ili kupata nafasi ndani ya kikosi cha kwanza kwa kuwa sijaja hapa kwa ajili ya kukaa benchi,”

Job amejiunga na Yanga akitokea ndani ya kikosi cha Mtibwa Sugar ya mkoani Morogoro aliyoichezea kwa mafanikio makubwa tangu mwaka 2016.

SOMA NA HII  KISA UJIO WA OKRAH....MOLOKO 'AKUTWA NA JAMBO' YANGA...