Home Yanga SC ALICHOSEMA CEDRIC KAZE BAADA YA KUFUTWA KAZI YANGA JANA

ALICHOSEMA CEDRIC KAZE BAADA YA KUFUTWA KAZI YANGA JANA


MASAA kadhaa baada ya Uongozi wa Klabu ya Yanga kumfungashia virago Kocha Mkuu wake Mrundi Cedric Kaze ametoa la moyoni baada ya uamuzi huo.

Kaze alitua Yanga kwa mbwembwe Oktoba mwaka jana, akichukua mikoba ya Zlatko Krmpotic ambayo na yeye imefikia ukomo jana akiwa Jijini Arusha.

Jana Yanga baada ya kulazimishwa sare ya bao 1-1 na Polisi Tanzania walitangaza kuliondoa benchi zima la ufundi huku wadau wengi wa soka wakimuonea huruma kocha msaidizi Nizar Khalphan ambaye alikuwa na muda mchache.

Kupitia mtandao wake wa kijamii, Instagram Kaze amesema ilikuwa furaha kubwa kufanya kazi na Yanga ndani ya miezi mitano toka kujiunga nao.

“Wananchi ilikuwafuraha kufanya kazi na nyie toka mieziu mitano michezo 18 ya ligi tumeshinda 10, sare saba, na kupoteza moja, mechi nne za Mapinduzi Cup na ndio mabingwa naiacha Yanga ikiwa nafasi ya kwanza nawatakia kila la kheri kwaherini,” ameandika Kaze.

Kaze ameongeza kuwa “Wananchi nimefurahi katika hii miezi mitano tumetumia pamoja, tumepata furaha na tukapata wakati mgumu lakini nyie subira iko ngumu kwa watu wengi,”amesema.

Aidha Kaze amesema anaondoka kifua mbele kwani mbali ya kukaa kwa furaha wamepitia furaha kwa kuwapatia kikombe cha kwanza amacho wamekikosa miaka mitatu mfululizo.

Hata hivyo tovuti ya Mwanaspoti Online imempigia Kaze kujua kinachoendelea juu yake baada ya uamuzi huo na kusema kuwa “Nimepokea hizo taarifa sawa, lakini kwa sasa naomba uniache nipumzike tuongee baadae,” amesema Kaze.

Mhamasishaji wa kikosi hicho, Antonio Nugaz amewataka Wanayanga kuwa watulivu wakati huu ambao uongozi unaendelea kulijenga benchi la ufundi jipya.

“Wanayanga msinung’unike, tembeeni vifua mbele, bado mnaongoza ligi, hata hao wanaosema na wao wanaviporo je wanajuaje kama vitalika,” amesisitiza Nugaz.

SOMA NA HII  YANGA YAMFUTA KAZI KOCHA WAO MKUU...KOCHA WA MUDA AKABIDHIWA TIMU