Home Yanga SC NYOTA HAWA SABA WA YANGA WASIPOCHUNGWA WATAWALIZA SIMBA

NYOTA HAWA SABA WA YANGA WASIPOCHUNGWA WATAWALIZA SIMBA

 

WAKATI Simba inayonolewa na Kocha Mkuu, Didier Gomes rekodi zikionyesha kuwa ni bora katika kila idara, bado kuna nyota wa Yanga nao wapo vizuri ikiwa hawatachungwa basi watawaliza wapinzani hao.
Vigogo hao wanatarajiwa kukutana Mei, 8 Uwanja wa Mkapa zikiwa zimebeki siku mbili, kwa upande wa kinara wa pasi za mwisho ni Clatous Chama wa Simba akiwa nazo 13 na amefunga mabao 7, rekodi ambazo hazijafikiwa na nyota yeyote ndani ya wapinzani wao Yanga.
Hawa hapa nyota 7 wa Yanga inayonolewa na Kocha Mkuu, Nassredine Nabi ambao ni wazuri katika rekodi na wasipochungwa watapeleka kilio Msimbazi namna hii kwa msimu wa 2020/21:-
Michael Sarpong
Nyota huyu aliwapa tabu Simba kwa kuanza kuwanyayua mashabiki wa Yanga mapema kipindi cha kwanza kwa penalti yake iliyomshinda mlinda mlango, Aishi Manula.
Licha ya kwamba hana kasi ya kucheka na nyavu akiwa na mabao manne na pasi mbili za mabao bado hapaswi kupuuziwa kwani anauwezo wa kubadili matokeo asipochungwa.
Yacouba Songne
Ni mtambo wa mabao ndani ya Yanga akiwa amehusika katika mabao 10 kati ya 41. Mabao 6 ametupia na pasi nne za mabao. Ni mzoefu katika mechi kubwa kwa sababu katika pasi nne za mabao alihusika kuiangamiza Azam FC kwa kumpa pasi mshikaji wake Deus Kaseke Uwanja wa Azam Complex wakashinda bao 1-0.
Amecheza jumla ya mechi 22 kati ya 27 ambazo timu yake imecheza kwa sasa.
Tuisila Kisinda

Mabao matatu na pasi mbili za mabao akiwa amecheza mechi 26 kati ya 27. Joash Onyango anakumbuka namna alivyokutana naye kwenye spidi na kusababisha penalti iliyofungwa na Michael Sarpong, Novemba 7, Uwanja wa Mkapa.
Tonombe Mukoko
Amehusika katika jumla ya mabao nane kati ya 41. Mabao manne na pasi nne katika mechi 25 ambazo amecheza ndani ya Yanga.Ni kiungo ambaye anapaswa kutazamwa kwa ukaribu.
 Ditram Nchimbi
Mshambuliaji huyu mzawa ni mwili jumba na nguvu nyingi uwanjani jambo ambalo limekuwa likimpa tabu beki Pascal Wawa katika kumzuia. Amecheza jumla ya mechi 21 amefunga bao moja na ana pasi mbili za mabao.
Carlos Carlinhos
Nyota huyu ni mzuri kwenye mipira iliyokufa akiwa na pasi tatu ambazo zote ilikuwa ni kwa kona zilizozamishwa nyavuni. Pia ametupia mabao matatu kibindoni na kumfanya ahusike kwenye mabao sita kati ya 41.
Wapinzani wake Simba wana kazi ya kumchunga Muangola huyu hasa katika mipira itakayokufa akipewa jukumu kuna jambo linaweza kutokea.
Saido Ntibanzokiza
Raia huyu wa Burundi anajeuri akiwa uwanjani na anajua kusoma mchezo. Amehusika kwenye mabao 7 kati ya 41 ambayo yamefungwa na Yanga. Mabao yake matatu na pasi nne zinaongeza nguvu kwa kikosi chake hivyo safu ya ulinzi ya Simba ina jukumu la kumchunga nyota huyu.
Chanzo:Championi

SOMA NA HII  KIKOSI CHA YANGA KITAKACHOANZA LEO DHIDI YA IHEFU