Home Azam FC KOMBE LA SHIRIKISHO LITAZAMWE KWA UMUHIMU, BURUDANI IENDELEE

KOMBE LA SHIRIKISHO LITAZAMWE KWA UMUHIMU, BURUDANI IENDELEE


 MASHABIKI ambacho kwa sasa wanahitaji ni kuona ushindani wa kweli kwenye mechi zote ambazo zinachezwa katika Kombe la Shirikisho la Azam Sports.

Ukiweka kando Ligi Kuu Tanzania Bara ambayo ipo kwenye lala salama kwa wakati huu pia Kombe la Shirikisho nalo ni miongoni mwa mashindano yenye mvuto mkubwa na yanafuatiliwa kwa ukaribu.

Ikumbukwe kwamba bingwa wa Kombe la Shirikisho anapata nafasi ya kuwakilisha Tanzania katika mashindano ya kimataifa yanayoandaliwa na Shirikisho la Soka Afrika, (Caf).


Hivyo ni muhimu kuanzia kwa wachezaji wenyewe kutambua kwamba wana kazi kubwa ya kufanya ili kupata ushindi na hawapaswi kupuuzia yale maelekezo ambayo wamepewa.


Jambo la msingi ni kila mchezaji kutambua ni lazima kwakwe kuwa na nidhamu nje ya mchezo na ndani ya uwanja. Ikiwa kila mmoja atakuwa makini ushindi utapatikana na kila mmoja atafurahi kile ambacho anakipata.


Kwa yule ambaye atashinda basi anapaswa kuanza maandalizi kuelekea kwenye mchezo wa fainali ambao huo ni wa maamuzi kwa nani ambaye atatwaa taji hilo.


Kwa mashabiki ambao watajitokeza uwanjani wanapaswa kuwa katika utulivu bila kuweza kuwa na makeke katika kuzipa sapoti timu zao.


Hivi karibuni imekuwa ikionekana kwamba mashabiki wanaojitokeza uwanjani wanaanzisha vurugu ambazo zinapoteza ule mvuto wa kujitokeza uwanjani hivyo wanapaswa kuzipa sapoti timu zao bila makelele.


Kwa upande wa waamuzi wao kazi yao ni moja kufuata sheria 17 ambazo wamepewa katika kusimamia maamuzi ili kuondoa zile changamoto ambazo zimekuwa zikitokea katika mechi za hivi karibuni.


Ikiwa wataweza kusimamia sheria hizo imani yangu ni kwamba hakutakuwa na malalamiko kwa wachezaji pamoja na mashabiki ambao watajitokeza uwanjani kuzipa sapoti timu zao.


Jambo liwe moja tu kwao kutenda haki ili hata mshindi ambaye atapatikana iwe ni kwa haki bila kelele kutoka kwa timu ambayo itashindwa kupata ushindi.


Hatutarajii kuona kwamba baada ya mchezo kuisha kunakuwa na suala la waamuzi kufungiwa kisa kuchezesha chini ya kiwango hilo hapana.


Hatua ya nusu fainali ambayo Biashara United na Yanga Azam FC na Simba zitacheza pamoja na fainali ambayo itawakutanisha washindi sio hatua ndogo ni kubwa na inahitaji umakini mkubwa.

SOMA NA HII  AZAM FC BADO WAPO IMARA


Kwa wachezaji rai yangu ni kuona kwamba kila mmoja anakuwa mlinzi wa mchezaji mwingine ili kuona kwamba hakuna ambaye anapata matatizo ndani ya uwanja.


Ikumbukwe kwamba mlinzi wa mchezaji uwanjani ni mchezaji mwenyewe ambaye anajua namna gani kila mmoja anakuwa katika harakati za kusaka ushindi.


Na washindi wasisahau kwamba wakipata nafasi ya kupeperusha bendera kimataifa kazi yao iwe kwenye kutafuta ushindi bila kuchoka kwa kuwa ni kwa manufaa ya Tanzania.


Nafasi nne ambazo zimepatikana zinapaswa kulindwa na timu zote ambazo zitapata fursa ya kucheza kimataifa msimu ujao ili tuwe tunatoa timu nyingi lakini zinakwenda kufanya vizuri pia.