Home news TFF YATOA TAMKO KUHUSU ISHU YA UCHAGUZI, ATHARI ZAKE NI KUFUNGIWA

TFF YATOA TAMKO KUHUSU ISHU YA UCHAGUZI, ATHARI ZAKE NI KUFUNGIWA


 UONGOZI wa Shirikisho la Soka Tanzania, (TFF) umewaomba wadau na wagombea kufuata kanuni za uchaguzi ambazo zimewekwa ili kuepuka athari ambazo zinaweza kuleta hasara kwa familia ya michezo.

Kwa sasa kuna mchakato wa uchaguzi unaoendela ndani ya TFF ambapo wagombea walirudisha fomu Juni 12 ikiwa ni siku ya mwisho kukamilisha mchakato huo na uchaguzi unatarajiwa kufanyika Agosti 7, Tanga.

Akizungumza na Waandishi wa Habari, leo Juni 14, Makao Makuu ya Shirikisho hilo, Karume, Katibu Mkuu wa TFF, Wilfred Kidao amesema kuwa hata wao hawana mamlaka ya kuingilia uchaguzi kwa kuwa wenye mamlaka ya kuzungumzia suala hilo ni Kamati ya Uchaguzi.

“Kumekuwa na malalamiko hivi karubini na nimekuwa nikipigiwa simu na waandishi wakihitaji kuniuliza kuhusu mchakato wa uchaguzi nimekuwa nikiwaambia kwamba wenye mamlaka ya kuzungumzia uchaguzi ni Kamati ya Uchaguzi.

“Ningependa kutoa rai kwa wagombea pamoja na wadau kufuata kanuni ambazo zimewekwa kuhusu uchaguzi na wenye mamlaka ya kufanya hivyo ni Kamati ya Uchaguzi hawa wanasimamia uchaguzi na sio sisi.

“Mchakato huu haupaswi kuingiliwa na ikiwa utaingiliwa utaleta athari kubwa kwa wanafamilia ya michezo jambo ambalo sio jema na hakuna mwanachama ambaye atapenda kuona haya yanafanyika.

“Katika kila hatua ambayo tunapitia tumekuwa tunawasiliana na Fifa. Hivyo ikitokea kukawa na muingiliano kuhusu mchakato basi kuna athari ambazo zitatokea mchakato utakapoingiliwa.

“Athari hizo ni pamoja na kusimamishwa uanachama athari ambayo kila mwanachama hapendi kuona inatokea. Unaposimamishwa maana yake ni kwamba timu ya taifa haitashiriki kwenye mashindano ya Fifa na Caf. Hata vilabu pia havitapata nafasi ya kushiriki mashindano ya kimataifa.

“Misaada inayotolewa na Fifa itasimamishwa. Rai yangu wadau wenye nia njema na mpira wa miguu ni bora wakafuata kanuni kuliko kuchukua hatua ambazo zitaathiri mpira wa miguu ambao umekuwa ni ajira,” amesema.

SOMA NA HII  JEMEDARI:- CHAMA AKIZIDIWA UWEZO UWANJANI ANAFANYAGA MAMBO YA KISHAMBA SANA...