Home Makala NYOTA HAWA WANA MAJINA MAKUBWA, ILA KAZI YAO UWANJANI KIDUCHU

NYOTA HAWA WANA MAJINA MAKUBWA, ILA KAZI YAO UWANJANI KIDUCHU


 KATIKA sekta ambayo ni pasua kichwa ni ile ya usajili kwa wachezaji hasa kutokana na kusubiri namna ambavyo wanaweza kujibu ndani ya uwanja.

Imekuwa kawaida wakati wa usajili wachezaji wengi wenye majina makubwa kuibwa na kupambwa ila mwisho wa siku namba ndani ya uwanja huwa zinakuwa ndogo mithili ya ‘pilitoni’.

Kwa muda huu ni muhimu kwa timu za Bongo kupambana kufanya usajili makini na utakaoleta tija lakini wanapaswa wajifunze kupitia makosa.

Hii ni orodha ya baadhi ya mastaa waliokuwa na majina makubwa zama za usajili ila namba zao kwenye utendaji zikawa za kishkaji kwa upande wa wachezaji wa kigeni:

Fiston Abdulazack

Alipotua Bongo, aliwaaminisha mashabiki kwamba atafanya kazi kubwa kwa kuwa anauzoefu wa mechi za kimataifa na zile za ushindani. Raia huyu wa Burundi alitabiriwa kuwa na pacha kali na Mrundi Said Ntibanzokiza ila mambo yakawa tofauti.

Ni bao moja alifunga ndani ya Ligi Kuu Bara ilikuwa mbele ya Polisi Tanzania na ngoma ilikuwa Polisi Tanzania 1-1 Yanga.

Pia kumbukumbu yake ya namba ilikuwa kwenye mchezo wa Kombe la Shirikisho, dhidi ya African Sports alipachika bao moja kwa mkwaju wa penalti. Hivyo ndani ya Yanga alitupia jumla ya mabao mawili.


Michael Sarpong

Raia huyu wa Ghana kilichomsibu ni yeye mwenyewe anajua kwa kuwa aliwahi kuliambia Championi Jumatatu kwamba anatambua mashabiki wanahitaji kuona yeye akifunga na hiyo ni kazi yake.

Ajabu kwenye namba ambazo aliziacha kwa msimu wa 2020/21 zilikuwa tifauti na mwili wake ambao umejengeka kimazoezi. Ni mabao manne ambayo alifunga ndani ya Yanga kati ya  mabao 52.

Rekodi zinaonyesha kwamba bao moja alifunga kwa penalti ilikuwa mbele ya watani za jadi, Simba, Uwanja wa Mkapa.

Perfect Chikwende

Ingizo jipya kwenye dirisha dogo ndani ya Simba akitokea Klabu ya FC Platinum ya Zimbabwe. Kumtungua kwake Aishi Manula kwenye Ligi ya Mabingwa kulimpa ulaji.



Alipoibuka Simba alipewa nafasi ya kufanya vizuri ila ngoma ilikuwa nzito kwake kwa mechi ambazo aliweza kucheza kuonyesha kile ambacho anacho.

SOMA NA HII  ORODHA YA WACHEZAJI WAPYA WA SIMBA AMBAO HUENDA WAKAISHIA KUKAA BENCHI AU JUKWAANI

Ni pasi moja ya bao ambayo alitoa kati ya mabao 78 ambayo yalifungwa na timu hiyo.

Junior Lokosa

Huyu alisajiliwa kwa mbwembwe ndani ya Simba na jina lake kubwa likapewa nafasi ya kufanya makubwa hasa kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika.

Hakuonekana kwenye mechi za Ligi ya Mabingwa Afrika na namba zake anatembea nazo kwenye miguu yake kwa kuwa alivunjiwa mkataba kimyakimya akasepa.

Mpiana Monzinzi

Nyota huyu raia wa Congo alikuwa anatajwa kwenda kumuongezea kasi Prince Dube katika utupiaji ndani ya Azam FC. Ngoma ilikuwa nzito alimaliza msimu akiwa amefunga mabao mawili pekee aliwafunga Gwambina FC.

Safari yake iliwadia kwa kuwa mabosi wa Azam FC waliachana naye.

Ally Niyonzima

Nyota huyu raia wa Rwanda bao lake la kwanza aliwatungua Mbeya City, Uwanja wa Sokoine, Mbeya na ana pasi moja ya bao huyu alipoibuka Azam FC alikuwa anatajwa kuingia pia kwenye rada za Yanga ila mambo yakawa tofauti.