Home news UNAAMBIWA ASUBUHI TU, WENYE NCHI WANAJAMBO LAO

UNAAMBIWA ASUBUHI TU, WENYE NCHI WANAJAMBO LAO



ZAMU ya Simba sasa baada ya Wananchi kukamilisha jambo lao. Kuelekea kwenye Simba Day inayotarajiwa kufanyika Septemba 19 wao wanasema kuwa One Team,One Dream, Asubuhi Tu, Twendeni Wenye Nchi.

Hii ni kauli mbinu inayotumika na Simba inayonolewa na Kocha Mkuu Gomes kuelekea kwenye tamasha lao maalumu la Simba Day.

Kuanzia Septemba 13 ni Wiki ya Simba kwa mashabiki kuweza kufanya matendo ya huruma kwa jamii. Hapa Championi Jumatano inakuletea namna mchongo mzima utakavyokuwa kwa timu hiyo iliyotwaa ubingwa msimu uliopita huku kiatu cha ufungaji bora kikiwa mikononi mwa nahodha John Bocco aliyetupia mabao 16.

Pia bao bora kwa msimu wa 2020/21 lipo mikononi mwa Bernard Morrison ambaye alifunga bao hilo mbele ya Namungo kwenye mchezo uliochezwa Uwanja wa Majliwa na Simba ilishinda mabao 3-1.

Kaimu Ofisa Habari wa Simba, Ezekiel Kamwaga aliliambia Championi Jumatano kuwa kila kitu kinakwenda sawa na wanatambua kwamba mashabiki watapata wanachokihitaji.

“Maandalizi kiujumla yanakwenda sawa na kila mchezaji yupo tayari kwa ajili ya msimu mpya. Kwa upande wa tiketi zipo tayari na zinauzwa huku jezi mpya zikiwa zinapatikana kwenye maduka ya Vunja Bei yote Tanzania,”.

Malengo ya Simba

Mwenyekiti wa Klabu ya Simba, Murtaza Mangungu aliliambia Championi Jumatano kuwa malengo makubwa ambayo yapo kwa sasa ni kufanya vizuri kwenye mashindano yote ambayo watashiriki.

“Tunahitaji kuchukua mataji yote ambayo tuliyatwaa msimu uliopita na hii inatokana na uwepo wa wachezaji wazuri, vifaa bora pamoja benchi la ufundi ambalo limejitosheleza,” .

TP Mazembe ndani

Kazi kubwa itakuwa ni kwenye kusaka ushindi kwenye mchezo wa kimataifa wa kirafiki kati ya Simba na TP Mazembe kutoka Congo.TP Mazembe inatarajiwa kushuka Dar Septemba 18 kwa ajili ya maandalizi ya mwisho ya mchezo huo.


Watakaokosekana

Wapo nyota ambao hawatakuwa ndani ya kikosi hicho kwa msimu mpya ikiwa ni Clatous Chama na Luis Miquissone. Viungo hawa walikuwa ni chaguo la kwanza la Gomes kwa sasa watakuwa katika changamoto mpya.

SOMA NA HII  ZA UHAKIKA HIZI....BAADA YA KUONA HAPATI NAMBA...KIPA SIMBA AVUNJA MKATABA...AKIMBILIA POLISI KUWEKA MAMBO SAWA..

Luis atakuwa ndani ya Al Ahly anakumbukwa kwa kuwa alipiga jumla ya pasi 10 za mabao na alifunga mabao 9 msimu uliopita huku Chama akifunga mabao 8 na pasi 13.


Mbali na hao pia kiungo Said Ndemla yeye atakuwa ndani ya Mtibwa Sugar sawa na Ibrahim Ame ambao wametolewa kwa mkopo huko.

Nyota wao Miraj Athuman ambaye alikuwa na kikosi msimu uliopita atakuwa ndani ya KMC kwa kuwa kandarasi yake ilimeguka na hakuongezewa.

Haji Manara, alikuwa ni Ofisa Habari wa timu hiyo na kwa sasa yupo zake ndani ya Yanga akiendelea kupeperusha bendera ya Wananchi.

Maingizo mapya

Mashabiki wengi watapata nafasi ya kuona maujuzi kutoka kwa nyota wao wapya ambao wamesajiliwa na timu hiyo ambayo kwa sasa ipo Arusha kwa ajili ya maandalizi ya msimu mpya wa 2021/22.

Miongoni mwa nyota ambao tayari wamemalizana na timu hiyo ni pamoja na Peter Banda ni ingizo jipya kutoka Big Bullet ya Malawi.Yusuph Mhilu, ingizo jipya kutoka Kagera Sugar huyu ni mshambuliaji.

Duncan Nyoni huyu ni raia wa Malawi alikuwa anakipiga Klabu ya Silver Strike. Pape Ousmane Sakho huyu ni kiungo kutoka Tenghueth ya Senegal.Henock Inoga Baka, huyu ni beki wanamwita beki wa kupanda na kushuka raia wa Congo.

Israel Mwenda ingizo jippya kutoka KMC, Abdul Samad, kutoka Kagera Sugar huyu ni kiungo. Emmanuel Mwanuke alikuwa anakipiga ndani ya Gwambina FC ya Mwanza.Sadio Kanoute, raia huyu wa Mali.

Benchi la ufundi

Hapa kuna ingizo jipya ambaye ni Hitimana Thiery raia wa Rwanda. Kocha huyu ana uzoefu na ligi ya Tanzania kwa kuwa aliwahi kuzifundisha timu mbalimbali Bongo ikiwa ni pamoja Mtibwa Sugar, Namungo na Biashara United.

Akiwa na Namungo aliweza kuipandisha mpaka Ligi Kuu Bara na alitinga nayo kwenye hatua ya Kombe la Shirikisho fainali na alipoteza kwa kufungwa mabao 2-0 dhidi ya Simba.