Home Makala BAADA YA KUTUA RUVU SHOOTING…ALLY SONSO ASIMULIA ALIVYOFUKUZWA YANGA..AMTAJA ZAHERA

BAADA YA KUTUA RUVU SHOOTING…ALLY SONSO ASIMULIA ALIVYOFUKUZWA YANGA..AMTAJA ZAHERA

 


WAKATI dirisha la usajali Bongo likifungwa, Klabu ya Ruvu Shooting ilitangaza kupata saini ya beki Ally Mtoni ‘Sonso’ kwa uhamisho huru akitokea Kagera Sugar.

Sonso ni miongoni mwa mabeki waliofanya vizuri nchini kutokana na kiwango ambacho alikionyesha akiwa na timu ya Lipuli FC ya mkoani Iringa, jambo lililowavutia mabosi wa Yanga kumsajili.

Idadi kubwa ya mashabiki walianza kumfahamu Sonso akiwa Lipuli, lakini ukweli ni kwamba beki huyo alianzia mchangani katika timu ya Kauzu FC.

Kauzu ni timu iliyopo Temeke, Dar es Salaam na imepata umaarufu kutokana na ushiriki wake wa mashindano ya Kombe la Ndondo.

Baada ya kupanda na kushuka kwa beki huyo, Mwanaspoti lilimtafuta na kupiga naye stori ambapo alieleza safari yake ya soka na mambo mbalimbali aliyokutana nayo.

MAISHA YA YANGA

Mtoni alijiunga na Yanga Desemba 2018 akitokea Lipuli ya Iringa, na beki huyo anasema maisha yake katika klabu hiyo yalikuwa mazuri, licha ya kutofikia malengo ambayo alijiwekea ya kuendelea kufanya vizuri kama mashabiki walivyokuwa wanamjua.

“Unapocheza klabu kubwa kama Yanga unakutana na mambo mengi kuanzia ndani na nje ya uwanja. Kila shabiki anataka ucheze kwa kiwango kikubwa bila kushuka kwenye kila mechi. Hali hiyo inasababisha kujikuta unakuwa na presha muda wote na kushindwa kufanya vizuri,” anasema.

KUONDOKA YANGA

Sonso anasema kuondoka kwake Yanga ilikuwa ni jambo la kuumiza katika maisha yake kwani aliamini kuwa bado ana nafasi ya kufanya vizuri na kuwaaminisha mashabiki kuwa uongozi wa Yanga haukukosea kumsajili.

“Nakumbuka siku moja niliitwa na kiongozi mmoja (jina tunalo) akaniambia anasitisha mkataba wangu, hivyo nitafute klabu nyingine ya kuchezea. Kwa kweli iliniuma sana, lakini nilichukulia kawaida tu kama changamoto za kimaisha,” anasema.

ZAHERA FRESHI TU

Beki huyo anasema katika maisha yake ya soka hatakaa amsahau aliyewahi kuwa kocha wa Yanga, Mwinyi Zahera baada ya kugundua kipaji chake na kuamua kumpeleka katika timu hiyo.

“Wakati nipo Lipuli tulicheza na Yanga na baada ya ile mechi Mwinyi Zahera akaniambia kijana una uwezo mkubwa sana, hivyo tutawasiliana,” anasema Sonso.

SOMA NA HII  MZIKI MZIMA WA SIMBA NA YANGA HUU HAPA

“Nikachukulia masihara, lakini kumbe alikuwa ana nia ya dhati ya kunisajili. Dili likakamilika na nikatimiza ndoto zangu za kucheza klabu kubwa hapa nchini, jambo ambalo sitakaa nilisahau moyoni mwangu daima.”