Home Ligi Kuu FT: YANGA 3-1 RUVU SHOOTING…. YANGA WAZIDI KUPIGWA BARIDI KALI KILELENI…

FT: YANGA 3-1 RUVU SHOOTING…. YANGA WAZIDI KUPIGWA BARIDI KALI KILELENI…


DAKIKA 90, zimemalizika katika Uwanja wa Benjamin Mkapa huku Yanga wakifanikiwa kuibuka na ushindi wa bao 3-1, dhidi ya Ruvu Shooting kwenye mchezo wa Ligi Kuu Bara.

Bao la Ruvu Shooting limefungwa na Shaban Msala dakika ya 8, kwa mpira ilopoteza mwelekeo uliomgonga beki Dikson Job na golikipa Djigui Diarra kubakia akidua kwani hakudhania mpira uliopigwa ungekuwa na madhara langoni mwake. Hii ni mara ya kwanza msimu huu kwa Yanga kuruhusu bao huku ikienda mapumziko bila ya ushindi.

Dakika ya 17, Yanga ilipanda nafasi ya wazi ya kusawazisha bao hilo baada ya mshambuliaji Yacouba Sogne kupiga shuti lililookolewa na golikipa Mohamed Makaka.

Dakika ya 24, ya mchezo nahodha wa Ruvu Shooting Santos Mazengo alipata kadi nyekundu baada ya kumfanyia madhambi mshambuliaji wa Yanga Fiston Mayele nje ya eneo la 18.

Kocha wa Ruvu Boniface Mkwasa alifanya mabadiliko ya kumtoa Marcel Kaheza na kumuingiza beki Ally Mtoni ili kuongeza nguvu kwenye eneo la ulinzi.

Mshambuliaji wa Yanga Yacouba Sogne alipata majeraha na kushindwa kuendelea na mchezo huku nafasi yake ikichukuliwa na Saido Ntibanzonkiza.Yanga iliendelea kulishambulia lango la Ruvu Shooting ambapo dakika ya 32, Feisal Salum ‘Fei Toto’ aliipatia Yanga bao la kusawazisha baada ya kupiga shuti kali nje ya 18, lililomshinda golikipa Mohamed Makaka.

Dakika ya 48 Djuma Shaban akaiandikia Yanga bao la pili kwa mkwaju wa penati baada ya Ally Sonso kuunawa mpira ndani ya boksi.

Yanga ilifanya mabadiliko kwa kumtoa Kibwana Shomari na kuingia David Bryson na Jesus Moloko akimpisha Farid Mussa. Dakika ya 76 Mukoko Tonombe ‘Ticha’ akapigilia msumari wa tatu baada ya kupigiwa bonge la pasi kutoka kwa Farid Mussa.

Kocha Nabi akafanya mabadiliko tena kwa kumtoa Feisal Salum Abdallah huku nafasi yake ikihukuliwa Yusuf Athuman na nafasi ya Mukoko Tonombe ikichukuliwa na Zawadi Mauya.

Kwa matokeo hayo, Yanga wanazidi kujikita kileleni mwa Ligi Kuu Bara wakiwa na jumla ya pointi 15 huku wakiwa wameshinda mechi zao zote tano ambazo wameshacheza mpaka sasa.

SOMA NA HII  BWANAEEH...KUMBE ISHU YA DIAMOND KUHAMIA YANGA UKWELI WAKE UKO HIVI...