Home news VUNJA BEI ATOA SHARTI LA KUIWEKA LOGO YA GSM KWENYE JEZI ZA...

VUNJA BEI ATOA SHARTI LA KUIWEKA LOGO YA GSM KWENYE JEZI ZA SIMBA…ATAKA TAARIFA TU….


Mzabuni wa Kubuni, Kuuza na Kusambaza vifaa vya michezo ya Klabu Bingwa Tanzania Bara Simba SC Kampuni ya VunjaBei imesema haijapokea agizo lolote la kuweka Logo ya Mdhamini Mwenza wa Ligi Kuu Tanzania Bara ‘GSM’, kwenye Jezi za za klabu hiyo.

Kauli hiyo ya Kampuni ya VunjaBei imetolewa na Mkurugenzi Mkuu Fred Nganjiro ‘VunjaBei’ alipozungumza na Waandishi wa Habari mjini Arusha jana Jumatano (Desemba 08).

Fred amesema mpaka sasa hajapokea taarifa zozote kutoka kwa viongozi wa Simba SC kuhusu agizo hilo, na kampuni yake inaheshimu mkataba waliousaini na klabu hiyo.

“Jezi sio mali ya Mzabuni, Jezi ni mali ya klabu, kwa hiyo sisi tunachokifanya, tunatengeneza jezi kutokana na masharti ambayo ninapewa na klabu.”

“Klabu ina Uongozi, Klabu ina Bodi ya Wakurugenzi, wao ndio wanasema VunjaBei jezi utakazotoa msimu huu weka NBC, GSM na Logo za makampuni mengine mimi ninaweka, lakini mpaka sasa Jezi ambazo zipo zimewekewa Logo za wadhamini kama nilivyoelekezwa na viongozi wa Simba SC.”

“Ambacho sijaambiwa na Uongozi sijaweka, kwa sababu hakuna makubaliano yoyote ambayo yananiruhusu kufanya hivyo, Jezi tulizozitengeneza hadi sasa mtaziona na Logo zilizopo zitaonekana.” amesema Fred VunjaBei.

Simba SC imeingia kwenye msuguano mkubwa na TFF, TPLB kufuatia agizo lililotolewa hivi karibuni kwa klabu za Ligi Kuu kuweka Logo ya Mdhamini Mwenza ‘GSM’ katika eneo la mkono wa kushoto wa jezi.

Uongozi wa Simba SC umesisitiza hautaweka Logo ya Mdhamini Mwenza ‘GSM’ hadi utakapotolewa ufafanuzi wa kina kuhusu mkataba uliosainiwa mapema mwezi Novemba.

Kampuni ya GSM ilisaini mkataba na TFF wa zaidi ya Shilingi Bilioni 2 kama Mdhamini Mwenza wa Ligi Kuu msimu huu 2021/22, huku Mdhamini Mkuu ni Benki wa Taifa ya Biashara ‘NBC’.

SOMA NA HII  KOCHA MPYA SIMBA SC APANIA MAKUBWA AFRIKA...HUO MSHAHARA WAKE KUFRU TUPU...