BAADA ya kusota kwa siku 213 bila kufunga hatimaye nahodha wa Simba, John Bocco ametakata kwa Mkapa.
Iko hivi Bocco mara ya mwisho kufunga ilikuwa Julai 18 mwaka jana dhidi ya Namungo katika ardhi ya Tanzania jana ameibuka tena baada ya kuifungia timu yake mabao 2 kati ya matano waliyoifunga Ruvu Shooting kipindi cha kwanza.
Simba walianza mchezo kwa kasi walitumia dakika mbili tu kuiadhibu Ruvu Shooting baada ya Yusuf Mhilu kumchongea pasi nzuri Bocco akiwa ndani ya box na kuunganisha mpira kwa kichwa.
Simba waliendeleza mashambulizi langoni mwa Ruvu Shooting dakika ya tatu na nane Bocco na Banda walishindwa kuwanyanyua mashabiki zao baada ya kushindwa kutumia nafasi walizotengenezewa.
Dakika ya 25 Clatous Chama ameongeza shangwe kwa mashabiki baada ya kuiandikia timu yake bao la pili akipokea pasi murua kutoka kwa Mzamiru Yassin.
Imemchukua dakika tatu tu Chama kuingia tena kambani akiifungia timu yake bao la tatu dakika ya 28 akitengewa pasi na Banda.
Bocco pamoja na kushindwa kutumia nafasi hakukata tamaa dakika ya 40 aliwanyanyua tena wanasimba wachache waliojitokeza kushuhudia mchezo huo.
Mashambulizi makali langoni kwa Ruvu Shootingi yalimchanganya beki Michael Masinda baada ya kuunganisha nyavuni krosi ya Gadiel dakika ya 45.