Home Habari za michezo BAADA YA KUKUBALI KICHAPO JANA…MBIVU NA MBICHI ZA STARS KUJULIKANA SEPT 3….WAKISHINDWA...

BAADA YA KUKUBALI KICHAPO JANA…MBIVU NA MBICHI ZA STARS KUJULIKANA SEPT 3….WAKISHINDWA TENA HAPO NDIO BASII…


TIMU ya Taifa Stars imeshindwa kutumia vyema Uwanja wa Benjamin Mkapa baada ya kufungwa bao 1-0 na Uganda katika mchezo wa kwanza wa kuwania nafasi ya kufuzu michuano ya Kimataifa kwa wachezaji wa ndani (CHAN) itakayofanyika Algeria mwakani.

Bao la Uganda liliwekwa nyavuni na Travis Mutyaba dakika ya 88, baada ya beki wa Stars, Mohamed Hussein ‘Tshabalala’ kupokonywa mpira wakati akiwa kwenye harakati za kuuokoa.

Kipindi cha pili Kocha wa Stars, Poulsen alianza kwa kufanya mabadiliko akiwatoa washambuliaji, Kibu Denis na George Mpole na kuwaingiza Tepsie Evans na Anwar Jabir.

Mabadiliko hayo yalionekana kuleta tija kwa kikosi cha Stars ambacho kilishambua lango la ‘The Cranes’ licha ya washambuliaji wake kukosa umakini mzuri wa kutumia nafasi zilizotengenezwa.

Poulsen aliendelea kufanya mabadiliko kwa kumtoa kiungo mshambuliaji, Farid Mussa na kumuingiza Daniel Lyanga ili kuongeza nguvu eneo la ushambuliaji ambalo lilionekana kushindwa kuonyesha makali.

Hata hivyo ubora wa mabeki wa ‘The Cranes’ wakiongozwa na John Revita ndio chanzo kikubwa cha kuwafanya washambuliaji wa Stars kuonekana kushindwa kupenya ngome hiyo akishirikiana na mwenzake Livingstone Mulondo.

Matokeo haya yanaifanya Stars kuwa na kibarua kigumu kwenye mchezo wa marudiano utakaopigwa Septemba 3, katika Uwanja wa St. Mary’s -Kitende uliopo Entebbe jijini Uganda.

Mshindi wa jumla baina ya miamba hii atafuzu moja kwa moja michuano hiyo itakayofanyika Algeria kuanzia Januari 13 hadi February 4, 2023.

SOMA NA HII  KISA RUVU SHOOTING KUFUNGWA NA YANGA...RAGE 'AJING'ATA ULIMI'... AFUNGUKA A-Z KILICHOTOKEA...