Home Habari za michezo BAADA YA KOCHA MBRAZILI KUTUA SIMBA SC…ISHU YA MGUNDA KUSEPA IKO HIVI…

BAADA YA KOCHA MBRAZILI KUTUA SIMBA SC…ISHU YA MGUNDA KUSEPA IKO HIVI…

Kocha Msaidizi Simba SC

Klabu ya Simba SC imemtambulisha rasmi Mbrazili, Robertinho Oliviera kuwa Kocha wao Mkuu mpya kwa mkataba wa miaka miwili.

Akizungumza na Waandishi wa Habari jijini Dar es Salaam, Mwenyekiti wa Klabu hiyo, Murtaza Mangungu amesema uzoefu wa Robertinho kwenye mashindano mbalimbali ndio sababu kubwa ya viongozi kumkabidhi jukumu hilo.

“Hakuna asiyejua alichokifanya katika timu mbalimbali alizofundisha na mfano mzuri tu ni kuifikisha hatua ya makundi Vipers kwa mara ya kwanza kwenye historia yao,” amesema Mangungu.

Kuhusu hatma ya Juma Mgunda ndani ya kikosi hicho, Mangungu amesema asingependa kuweka wazi juu ya hilo ingawa mashabiki na wadau wanapaswa kutambua bado ni mwajiri wao na ataendelea na majukumu yake kama kawaida.

Kwa upande wa Robertinho amesema moja ya malengo yake makubwa ni kuifikisha Simba SC hatua ya nusu fainali kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika na Ikiwezekana hadi fainali.

“Nina furaha kujiunga hapa na ni matumaini yangu nitaendelea kusimamia malengo yaliyowekwa na Klabu, Simba SC ina wachezaji wakubwa na wazoefu hivyo naamini kwa umoja wetu tutafanikiwa,” amesema na kuongeza;

“Watu walisema mambo mengi sana wakati nikiwa Vipers kwamba sitoweza kuitoa TP Mazembe lakini wanashindwa kuelewa kila kitu kinawezekana kwenye Mpira wa Miguu.,”

Akiwa na Vipers, Robertinho aliiongoza katika michezo 58 ya mashindano yote ambapo kati ya hiyo ameshinda 43, sare tisa na kupoteza sita tu akifanikiwa kutwaa mataji mawili ya Kombe la Uganda na la Ligi Kuu nchini humo.

Mbali na mataji hayo ila Robertinho alikuwa Kocha bora wa msimu huku akiiwezesha Vipers kutinga hatua ya makundi kwenye Ligi ya Mabingwa Afrika kwa mara ya kwanza katika historia ya Klabu hiyo.

SOMA NA HII  MUDATHIR AVUNJA UKIMYA AZAM...AFUNGUKA KINACHOWAKWAMISHA..WACHEZAJI NA KOCHA WATAJWA..