Home Habari za michezo BAADA YA KUJIUNGA NA YANGA…MUDATHIRI ATAJA NAFASI ZA AUCHO NA SURE BOY…

BAADA YA KUJIUNGA NA YANGA…MUDATHIRI ATAJA NAFASI ZA AUCHO NA SURE BOY…

Habari za Yanga SC

Wakati Khalid Aucho juzi alisaini mkataba mpya wa miaka miwili wa kuendelea kuitumikia Yanga SC na kuzima uvumi wa kutakiwa na klabu nyingine, kiungo mpya wa timu hiyo, Mudathir Yahya amefunguka kuwa anajiamini na anahitaji nafasi aonyeshe utofauti wake na waliopo.

Aucho na Mudathir wote wanacheza nafasi moja ya kiungo mkabaji na sasa inaonekana kutakuwa na vita kwenye kuwania nafasi hiyo.

Mudathir ambaye alikuwa nje ya uwanja kwa miezi sita baada ya kuachwa na waajiri wake wa zamani Azam FC amejiunga na Yanga kwa mkataba wa miaka miwili na amesema yupo fiti kupambana.

Akizungumza Mudathir alisema anafahamu Yanga SC ina kikosi kizuri na cha ushindani kutokana na uwepo wa mastaa wengi ambao wameweza kuipambania timu hiyo, lakini anaamini na yeye akipewa muda ana kitu chake cha tofauti cha kuonyesha.

“Nilikuwa nje ya uwanja kwa muda huo haina maana kwamba nilikuwa sifanyi mazoezi, nilikuwa na timu ya KMKM ambayo nilifanya nayo mazoezi, niko fiti hata muda huu nikipewa mechi nacheza,” alisema Mudathir na kuongeza;

“Wachezaji tunafahamiana kila mmoja ana umuhimu wake kwa nafasi yake, sikatai Yanga SC kuwa ina viungo wengi, hii hainifanyi na mimi nikaamini kuwa siwezi kucheza, nimefanya uamuzi sahihi kusaini mkataba ninaamini katika uwezo na kipaji nilichonacho.”

Akizungumzia kuhusu Ligi Kuu Bara alisema ana uzoefu wa kutosha akicheza timu mbili tofauti akiwa Azam FC na Singida United, hivyo hana anachokihofia huku akitaja mashindano ya kimataifa ambayo Yanga wanashiriki hatua ya makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika, alisema pia ana uzoefu na mashindano haya.

“Ligi Kuu haibadiliki, kinachobadilika ni wachezaji nina uzoefu nayo, nimejiandaa kwenda kuipambania timu kuhakikisha inatetea taji na kuhusu kimataifa nina nafasi ya kucheza kwa sababu msimu huu sijashiriki nikiwa na timu yoyote.”

Mudathir anaweza kucheza nafasi mbili uwanjani akimudu kucheza kiungo mkabaji anayocheza Aucho na kiungo mshambuliaji na sasa anaungana na Salum Abubakar ‘Sure Boy’ waliyecheza pamoja Azam FC.

SOMA NA HII  UBABE WA MBAPPE KWENYE MAGOLI UNAVYOBAMBA NA MAOKOTO YA MERIDIANBET...