Home Habari za michezo HII HAPA SABABU YA GEORGE MPOLE KUBAKI SEBULENI CONGO WAKATI TIMU YAKE...

HII HAPA SABABU YA GEORGE MPOLE KUBAKI SEBULENI CONGO WAKATI TIMU YAKE IKICHEZA….

Mpole Congo

Nyota wa zamani wa Geita Gold na Mfungaji Bora wa Ligi Kuu Bara msimu uliopita, George Mpole aliyesajiliwa na FC Lupopo ya DR Congo usiku wa kuamkia jana aliishia kukaa sebuleni kuiangalia timu yake mpya ikitupa karata ya kwanza ya mechi za makundi ya Kombe la Shirikisho Afrika dhidi ya USM Alger ya Algeria.

Lupopo ilikuwa ugenini mjini Algers kuvaana na wenyeji kwenye mechi ya Kundi A la michuano hiyo, huku Mpole aliyefunga mabao 17 msimu uliopita akiwa na Geita na kubeba tuzo akimzidi bao moja kinara wa sasa, Fiston Mayele wa Yanga alikuwa sebuleni kucheki mchezo huo.

Straika huyo tayari jina lake lilishatumika kwenye michuano hiyo akiwa na Geita iliyotolewa raundi ya awali na Hilal Alsahil ya Sudan kwa faida ya bao la ugenini baada ya matokeo ya jumla kuwa mabao 2-2, Geita ikilala ugenini 1-0 na kushinda nyumbani 2-1.

Licha ya kuukosa mchezo huo, Mpole alisema kujiunga kwake na Lupopo kumemfungua macho kwa mambo mengi na kubwa ni aina ya ushindani wa namba aliokutana nao aliosema unazidi kumkuza zaidi katika maisha yake ya soka.

“Kila timu ina ushindani mkali, nimepata nafasi nzuri ya kuwasoma ubora wa wenzangu, ili nikianza majukumu yangu kwenye ligi nijue pakuanzia,” alisema Mpole na kuongeza;

“Najiona nina kazi kubwa ya kuifanyia timu hii kwani wakati natambulishwa niliona wengi wanaonyesha matumaini makubwa na mimi, wachezaji na benchi la ufundi, hilo linanifanya nijitume sana mazoezini.”

Alisema tangu ajiunge na timu hiyo, amejifunza jinsi ya kuzitazama nyakati kwa umakini na kuhakikisha anafanya vitu ambavyo vitaacha kumbukumbu kwa wengine kujifunza upambanaji.

“Mfano mazoezi ya timu hii, kila mchezaji anapambana utadhani anafanya majaribio ya kuonekana pia wanathamini sana muda wa kufanya vitu vya msingi.

“Natambua soka lina wakati, hivyo wakati nilionao ndio wa kufanya vitu kwa bidii ili zikipita ziwe na kumbukumbu nzuri ya wengine kujifunza mambo mbalimbali kutoka kwangu na kwa wengine.”

SOMA NA HII  KWA HALI JINSI ILIVYO...YANGA WAKIZUBAA KIDOGO TU ..IMEKULA KWAO MAZIMA...ISHU IKO HIVI 'MWAMBA'...