Home Habari za michezo YANGA WAGOMA KUTANGAZA KIKOSI CHAO…WABAKISHA WAWILI HAWA USAJILI MPYA

YANGA WAGOMA KUTANGAZA KIKOSI CHAO…WABAKISHA WAWILI HAWA USAJILI MPYA

Habari za Yanga

Yanga hawataki kukifumua kikosi chao katika msimu ujao, na sasa wamebakiza wachezaji wawili kati ya watatu waliopanga kuwaongeza katika usajili wa msimu ujao.

Timu hiyo, tayari imekamilisha usajili wa winga matata na hatari wa TP Mazembe ya Lubumbashi huko DR Congo, Phillipe Kinzumbi baada ya kufikia makubaliano mazuri ya pande hizo mbili.

Kiungo mshambuliaji wa Singida Big Stars, Mbrazil Bruno Gomes ni kati ya wachezaji wanaotajwa kujiunga na Yanga katika msimu ujao.

Mmoja wa mabosi wa timu hiyo, amesema kuwa wamepanga kusajili wachezaji kuanzia wawili hadi watatu pekee katika usajili wao wa msimu ujao.

Bosi huyo alisema kuwa hawaoni sababu ya kuongeza wachezaji wengi katika usajili huo, kwani kikosi chao kila idara ina wachezaji kuanzia wawili ambao wote wana nafasi ya kucheza katika kikosi cha kwanza.

Aliongeza kuwa nafasi walizopanga kuzifanyia maboresho ni kiungo mchezeshaji mwenye uwezo wa kupiga pasi za mwisho ambaye anatajwa Gomes na mawinga wawili wenye kasi tayari mmoja amepatikana ambaye ni Kinzumbi.

“Hatuoni sababu ya kujaza wachezaji wengi katika usajili wetumkubwa, hivyo tumepanga kusajili wachezaji kuanzia wawili hadi watatu wenye uzoefu na uwezo wa kucheza michuano ya kimataifa.

“Katika kikosi chetu wapo wachezaji wengi wenye viwango bora ambao wamekuwa hawapati nafasi ya kucheza kutokana na ushindani wa namba ambao wanaupata kutoka kwa wenzao, hivyo hatuoni sababu ya kusajili wengine wapya hasa wazawa.

“Kwani hivi sasa uongozi unafikilia kufika mbali kimataifa, hivyo usajili wetu utaangalia ubora na uzoefu wa kucheza michuano ya kimataifa, kwani malengo yetu ni kubeba taji kubwa Afrika.

“Tayari wapo wachezaji tuliokuwa katika mipango yetu kwa ajili ya kuwasajili katika msimu ujao, kati ya hao yupo Kinzumbi ambaye yeye dili lake limekamilika kwa asilimia kubwa,” alisema bosi huyo.

Rais wa timu hiyo, Injinia Hersi Said hivi karibuni alizungumzia hilo la usajili na kusema:

“Usajili wetu unasimamiwa na kocha wetu Nabi (Nasreddine) ambaye yeye ndio anatoa mapendekezo ya wachezaji anaowahitaji.

“Mara baada ya kupendekeza, linafuata suala la utekelezaji kwa uongozi, Yanga hatuingilii usajili katika benchi letu la ufundi.”

SOMA NA HII  MANARA ATUA MAKKAH, AWAOMBA WATANZANIA JAMBO HILI