Home Habari za michezo KUHUSU ISHU YA MAZEMBE KUMNG’ANG’ANIA BALEKE…SIMBA WAIBUKA NA KUANIKA KILA KITU WAZI…

KUHUSU ISHU YA MAZEMBE KUMNG’ANG’ANIA BALEKE…SIMBA WAIBUKA NA KUANIKA KILA KITU WAZI…

HABARI ZA SIMBA

Wakati kukiwa na tetesi za mshambuliaji wa Simba SC, Jean Baleke, kutakiwa na klabu ya Ulaya, mabosi wa Wekundu wa Msimbazi wamesema nyota huyo ni mali yao na timu yoyote inayomhitaji, itatakiwa kufuata taratibu.

Simba SC ilimsajili Baleke kwa mkataba wa mkopo wa miaka miwili akitokea TP Mazembe ya Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo (DRC), na kwa kipindi kifupi ameisaidia timu hiyo katika michuano mbalimbali.

Meneja wa Habari na Mawasiliano wa Simba SC, Ahmed Ally, amesema Baleke ana mkataba na klabu yao na kwa sasa wao ndio wanaotakiwa kutoa baraka kwa timu nyingine itakayojitokeza kuhitaji huduma ya Mkongomani huyo.

Ahmed amesema endapo TP Mazembe wamepokea ofa ya kumhitaji mshambuliaji huyo, mabingwa hao wa zamani watalazimika kufanya mazungumzo na Simba SC kuhusu mchakato huo na hatimaye kufikia makubaliano.

“Ni kweli Baleke yuko Simba SC kwa makubaliano maalum ambayo tumefanya na TP Mazembe, lakini endapo kuna ofa imewafikia wanatakiwa kutuambia na kama watamuuza bila kutujulisha watalazimika kurejesha fedha zetu kulingana na makubaliano tuliyoingia,” amesema Ahmed

Ameongeza Simba SC inatakiwa kushirikishwa juu ya mauzo ya nyota huyo ila kwa sasa wanatambua bado ni mchezaji wao halali kutokana na mkataba ambao walikubaliana na TP Mazembe.

“Kuhusu TP Mazembe kupokea barua ya ofa hatuna taarifa nayo, kwa sasa siwezi kuweka wazi kwa sababu taarifa hizo bado hazijafikia mezani kwangu, tutaweka wazi taarifa juu ya ofa hiyo ya Baleke kuondoka Simba muda útakapofika,” Ahmed amesema

Baleke aliyejiunga Simba SC katika dirisha dogo amefunga mabao nane wakati kinara ni Fiston Mayele wa Young Africans ambaye amezifumania vyavu za wapinzani mara 16.

SOMA NA HII  KISA SIMBA NA YANGA...WADHAMINI LIGI KUU WAIBUKA NA HOJA MPYA...WAWEKA WAZI VIAUMBELE VYAO...