Home Habari za michezo ALPHONCE MABULA MBONGO ANAYESUMBUA ULAYA…WAZUNGU WAMFANANISHA NA TRENT WA LIVERPOOL..

ALPHONCE MABULA MBONGO ANAYESUMBUA ULAYA…WAZUNGU WAMFANANISHA NA TRENT WA LIVERPOOL..

Habari za Michezo

NYOTA wa Kitanzania, Alphonce Mabula ambaye anacheza soka la kulipwa Serbia akiwa na FK Spartak Subotica ya ligi kuu ‘Serbian SuperLiga’ ametajwa kuwa anaweza kufika mbali.

Anachotakiwa kufanya kwa sasa ni kuendelea kupambana huku akisubiri milango ya mafanikio yake kufunguka hayo ni maneno ya kocha wa kikosi hicho, Aleksandr Kerzhakov ambaye enzi zake alitamba akiwa na Zenit Saint Petersburg ya Russia na Sevilla ya Hispania.

Kerzhakov ambaye alikuwa mshambuliaji hatari kabla ya kugeukia ukocha, anasema,”Ni mchezaji mwenye nguvu na maarifa, napenda sana namna ambavyo amekuwa akijituma, anakitu na namwona mbali miaka michache ijayo, anatakiwa kuendelea kupambana maana maisha ya mpira ni mapambano.”

Alphonce mwenye miaka 20 yupo kikosi kimoja na Morice Abraham ambaye anaye anatajwa kuwa na kipaji cha kipekee.

“Kila kitu kipo mikononi mwao, kuwa na kipaji pekee siku hizi haitoshi wanatakiwa kujitoa na kupigania nafasi ya kucheza mara kwa mara,” anasema kocha huyo ambaye alikuwa mfungaji bora wa Ligi Kuu Russia, 2004.

Hatukuishia hapo, tulifanya mawasiliano na Alphonce ambaye hapa anafunguka maisha ya Serbia na ilikuwaje hadi kupata nafasi ya kucheza soka la kulipwa nchini humo ambako ni nyumbani kwa mshambuliaji hatari wa Juventus, Dusan Vlahovic.

“Maisha ya Serbia mazuri na ligi yake pia ni nzuri changamoto iliyopo ni hali ya hewa, ikiwa kipini cha baridi ni baridi kwelikweli mabarafu yanamwagika na inabidi uende hivyo hivyo mazoezini na kucheza mechi hivyo hivyo na ikiwa kiangazi kama saivi ni jua kali sana,”

“Jua la huku huwa naona kama kali kuliko la Dar, ambacho kinatusaidia mimi na mwenzangu ni uvumilivu tuna ndoto ambazo tunazipambania hivyo hatupo tayari kurudi nyuma,” anasema kinda huyo.

Anaendelea kwa kusema,”Najivunia kuwa hapa na nashukuru sana namna ambavyo wachezaji wenzetu hasa wakubwa kwenye timu vile wamekuwa wakitusaidia kuhakikisha tunaendana nao ili kuisaidia timu, wamekuwa wakinifananisha na Trent (Alexander-Arnold) wa Liverpool.”

Ilikuwaje akapata shavu la kucheza soka la kulipwa Serbia, Alphonce anasimuliwa kwa kusema,”Safari yangu ilianzia kwenye akademi ya Alliance ya Mwanza nimekulia pale, nilibahatika kupata nafasi timu ya taifa chini ya miaka 15 nikaendelea kukua hadi chini ya miaka 17,”

“Nashukuru Mungu nilikuwa sehemu ya wachezaji ambao walichaguliwa kwa ajili ya Afcon 2019 chini ya miaka 17 mashindano yaliyofanyikia nyumbani Tanzania baada ya apo nilipandishwa timu ya wakubwa Alliance msimu ule ilikuwa ligi kuu nikapata nafasi kucheza ligi kuu.”

Alphonce anasema baada ya hapo aliitwa kwenye kikosi cha timu ya taifa chini ya miaka 20 iliyoenda kucheza Afcon Maurtania ndipo alipokutana na ajenti ambaye alimsaidia kupata nafasi Serbia.

“Niliskautiwa na meneja wangu wa saivi anaenisimamia Berna Erasmus ambaye yupo ubeligiji. Akanitafutia timu Serbia nikaenda kufanya majaribio ambayo yalikuwa ya wiki moja, walinipitisha na nilikuwa tayari na miaka 18 nikasaini mkataba wangu wa kwanza kama mchezaji wa kulipwa katika timu yangu ya Spartak Subotica ambayo ndo nipo bado hadi kwa sasa,” anasema.

Malengo yake ni yapi? Alphonce anasema,”Malengo yangu ni kupiga hatua na kusogea zaidi kweny ligi tano bora za ulaya ili nizidi kusogelea ndoto yangu ya kucheza Ligi Kuu England hiyo ndo ndoto yangu kubwa nayoiwaza kila siku kichwani mwangu naamini inawezekana.”

Nahodha wa Taifa Stars, Mbwana Samatta ambaye kwa sasa anaichezea PAOK ya Ugiriki ndiye mchezaji wa Kitanzania anayeshikilia rekodi ya kucheza na kufunga kwenye ligi ya England ambayo Alphonce anatamani kucheza siku moja.

“Nimekuwa nikipata nafasi ya kuzungumza na Samatta na amekuwa akitupa moyo kuwa inawezekana kucheza kwenye ligi kubwa barani Ulaya, amekuwa mfano mzuri kwetu na vijana wengine ambao wanachipukia,” anasema.

SOMA NA HII  ZA NDAANI KABISA....KABLA GIZA HALIJAWA KALI...VIFAA HIVI VIPYA KUTIA NANGA YANGA....YUPO MBURUNDI WA UINGEREZA...