Home Azam FC SIO SIMBA,YANGA WALA AZAM HAWACHEKANI TENA MAANA MABO YENYEWE YAPO HIVI

SIO SIMBA,YANGA WALA AZAM HAWACHEKANI TENA MAANA MABO YENYEWE YAPO HIVI

NGAO ya jamii inahusisha timu nne kwa mara ya kwanza kuanzia imeanzishwa hapa nchini na kipute chake ni kuanzia Agosti 9 hadi 13.

Ni michezo ambayo mashabiki wa soka wanaisubiri kwa hamu kubwa kutokana na majembe mapya ambayo yamesajiliwa na timu zao.

Timu zinazoshiriki michuano hiyo ni Simba, Yanga, Azam na Singida Fountain Gate na Simba itacheza na Singida na Azam dhidi ya Yanga na mshindi wa michezo hiyo ya kwanza zitakutana kwenye fainali Agosti 13.

Hapa ndiyo mastaa wataanza kuonyesha makali yao waliyotua nayo kutoka kwenye mataifa mbalimbali.

Hata hivyo, usajili mpya wa msimu huu umeonekana kuziwekea mtego timu kubwa tatu, kutokana na zote kufanana kwenye aina ya usajili ambao zimefanya.

Ni adimu jambo moja kutokea kwa timu za Simba, Yanga na Azam kwa wakati mmoja, lakini kwa msimu huu kwenye usajili timu hizo mambo yamekuwa sare sare.

Kwenye usajili wa majina mapya ya msimu huu hadi sasa Simba wamesajili kutoka kwenye nchi nne tofauti na wamesajili wachezaji wawili kutoka Cameroon, ambao ni Che Malone na Willy Onana.

Lakini wamemchukua mchezaji mmoja kutoka Ivory Coast, Kramo Aubin, wakamchukua Luis Missquinne kutoka Msumbiji pamoja na Fabrice Ngoma ambaye ni mzaliwa wa Congo.

Hata hivyo, Simba wanaweza kuongeza mchezaji kutoka taifa lingine kwa kuwa bado hajamaliza suala la kipa baada ya awali kumleta Mbrazili na kuamua kumvunjia mkataba kwa madai anasumbuliwa na majeraha ya muda mrefu.

Hata hivyo, Azam nao wamefanya usajili wao kutoka kwenye mataifa manne makubwa ya soka Afrika sawa na ilivyofanya Sim-ba, lakini wenyewe wakisajili kutoka nchi ya Senegal, wachezaji wawili kama Simba walivyofanya kutoka Cameroon.

Wenyewe wamemsajili Allasane Diao na Cheikh Sidibe ambao ni raia wa nchi hiyo inayoongoza kwa ubora wa soka Afrika, pia wakiwa wamemsajili mchezaji mmoja kutoka Gambia Gibril Sillah, lakini wakaenda DR Congo na kumaliza kwa kumsajili Yanick Bangala ambaye ameuzwa kutokea Yanga.

Mfanano wa Azam na Simba ni kutoa wachezaji wao kwenye mataifa manne tofauti, lakini wakiwa wametoa wachezaji wawili kutoka nchi moja kama ambavyo Simba walifanya kwa kusajili Wacameroon wawili.

Kwa upande wa Yanga wenyewe wamekuwa na tofauti kwenye nchi ambazo wamechukua wachezaji baada ya kusajili kutoka kwenye mataifa sita, tofauti na Simba na Azam ambao wamesajili kutoka kwenye mataifa manne.

Lakini kuonyesha kuna jambo wamefanya kama pacha, Yanga nao wana wachezaji wawili ambao imewasajili kutoka kwenye taifa moja, nalo ni Ivory Coast, sehemu ambayo wamekwenda wakamchukua kiungo mshambuliaji, Pacome Zouzoua na beki wa pembeni Yao Kouassi.

Hii ni picha halisi kwenye dirisha moja la usajili timu zote tatu ambazo zilimaliza kwenye tatu bora msimu uliopita zimesajili wachezaji wawili kila moja kutoka kwenye taifa moja, lakini kumbuka Yanga imepunguza kundi kubwa la Wacongo ambao ilikuwa nalo msimu uliopita.

Mbali na taifa hilo, wengine ambao Yanga imewasajili hadi sasa ni Maxi Nzengeli kutoka DR Congo pamoja , Gift Fred kutoka Uganda na Scudu Makudubela kutoka Afrika Kusini akiwa ni mchezaji wa kwanza kutoka nchi hiyo kucheza nchini.

Lakini bado wakasogea na kwenda Ghana ambapo walimsajili mshambuliaji Hafiz Konkoni ambaye kwenye timu hiyo ndiyo mchezaji wa mwisho kufunga usajili.

MABEKI

Jambo lingine ambalo limeonekana kuwa la mfanano kwa timu hizo ni zote zimesajili mchezaji anayecheza beki wa kati ambapo Simba wameshusha Che Malone na Yanga wamemsajili Fred, huku Azam wao kama hawatamtumia Bangala kwenye eneo la kiungo wanaweza kumtumia kama beki wa kati, lakini wakiwa wamemsajili Sidibe pia kwenye eneo hilo.

MAWINGA

Inaonekana makocha wa timu zote mbili Simba na Yanga walikuwa na tatizo kwenye eneo la mawinga na wote wamesajili wachezaji wa sehemu hizo zote.

Simba wamemsajili Luis anayeweza kucheza eneo la winga ya kushoto, pia wakimsajili Onana anayeweza kucheza pia eneo la winga ya kulia na mshambuliaji wa kati.

WASHAMBULIAJI

Timu zote tatu za Simba, Yanga, Azam pamoja na msimu uliopita kufanya vizuri kwa kufunga mabao mengi, lakini zote zimefanya usajili wa mshambuliaji wa mwisho.

Azam wao wamemsajili mshambuliaji, Alassane Diao, Yanga wakihaha hadi mwishoni na kumnasa Konkoni huku Simba wao mapema sana wakikamilisha usajili wa mshambuliaji wa mwisho Onana ambaye anaweza pia kucheza pembeni.

SOMA NA HII  YANGA WAITAKA REKODI HII MPYA AFRIKA