Home Habari za michezo SIRI YA SIMBA KUMSAJILI AYOUB KAMA KIPA WAO MPYA YAFICHUKA

SIRI YA SIMBA KUMSAJILI AYOUB KAMA KIPA WAO MPYA YAFICHUKA

Habari za Simba leo

Kigezo cha uzoefu wa mashindano ya kimataifa, kimeonekana kuwa sababu kuu iliyoishawishi Simba kumsajili kipa Ayoub Lakred kutoka FAR Rabat ya Morocco ambaye leo klabu hiyo imemtambulisha rasmi kama usajili wao mpya msimu huu.

Kipa huyo mwenye umri wa miaka 28 raia wa Morocco, amecheza idadi ya mechi 16 za Kombe la Shirikisho Afrika ambazo ameruhusu nyavu zake kutikiswa mara 12 na michezo nane alimaliza bila kufungwa bao.

Mbali na Kombe la Shirikisho Afrika, kipa huyo mwenye urefu wa Mita 1.86, amecheza mechi moja ya mashindano ya Klabu Bingwa kwa timu kutoka nchi za Kiarabu, mechi 97 za Ligi Kuu ya Morocco na mechi sita za Kombe la Throne.

Katika mechi 97 za Ligi Kuu ya Morocco ambazo amecheza, Lakred ameruhusu nyavu zake kutikiswa mara 81 huku akicheza mechi 38 bila kufungwa bao.

Simba imemsajili Lakred kwa ajili ya kuwaongezea nguvu Ally Salim, Hussein Abely na Feruzi Telu katika kipindi hiki ambacho inamkosa kipa wake chaguo la kwanza Aishi Manula na alitambulishwa leo saa 7:00 mchana na klabu hiyo.

“Karibu Msimbazi, Ayoub Lakred,” iliandika Simba katika ukurasa wake wa Instagram.

Lakred anakuwa mchezaji wa 11 kusajiliwa na Simba katika dirisha hili kubwa la usajili wengine wakiwa ni Che Malone, Henock Inonga, David Kameta, Luis Miquissone, Willy Onana, Aubin Kramo, Hamis Abdallah, Shaban Chilunda, Hussein Abely, Hussein Kazi na Fabrice Ngoma.

SOMA NA HII  NABI AITABIRIA MAKUBWA YANGA YA GAMONDI