Home Habari za michezo BAADA YA KUPATA DILI JIPYA…,MSUVA AFUNGUKA A-Z KINACHOMFELISHA UARABUNI…

BAADA YA KUPATA DILI JIPYA…,MSUVA AFUNGUKA A-Z KINACHOMFELISHA UARABUNI…

Saimon Msuva

Mshambuliaji Saimon Msuva amesema hataruhusu historia ya kucheza soka la kulipwa Saudi Arabia kwa muda mfupi ijirudie akitambia kubebwa na uzoefu wa soka na mazingira ya nchini humo ambako ataelekea siku chache zijazo.

Nyota huyo wa timu ya taifa ‘Taifa Stars’ hivi karibuni alikamilisha kujiunga na Al Najmah inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza nchini humo akiwa mchezaji huru baada ya kuachana na JS Kabylie ya Algeria.

Hii ni mara ya pili kwa Msuva kucheza soka la kulipwa nchini humo ambapo mara ya kwanza aliitumikia Al-Qadsiah inayoshiriki Ligi Daraja la Kwanza kama Al Najmah.

Hata hivyo, hakudumu sana Al-Qadsiah ambapo aliichezea msimu mmoja kabla ya kuachana nayo na kujiunga na Kabylie ambayo hivi karibuni alivunja mkataba.

Msuva alisema anaamini kilichotokea nyuma hakitajirudia safari hii kwani tayari ana uzoefu wa soka la Saudi Arabia na maisha kwa ujumla.

“Malengo yangu ni kucheza kwa muda mrefu kule Saudi Arabia. Sina wasiwasi na hilo kwa sababu naifahamu vyema ile Ligi Daraja la Kwanza na nilishacheza. Nilicheza pale kwa msimu mmoja na bahati mbaya uongozi wa timu ulibadilika hivyo sikuweza kuendelea ingawa nilitamani kucheza kwa muda mrefu zaidi,” alisema.

“Lakini kwa sasa nina uzoefu wa kule na nimejiandaa kuhakikisha malengo yangu yanatimia. Kikubwa sio ligi nyepesi hivyo jambo la msingi ni kupambana ili kuweza kuisadia timu yangu.”

Mshambuliaji huyo alisema anatamani kuona wachezaji wengi wa Kitanzania wanatoka kwenda nje ya nchi kucheza ili waimarike na kuwa bora zaidi kwa ajili ya kuisaidia Stars katika mashindano mbalimbali inayoshiriki.

Katika hatua nyingine, Msuva alisema anatamani kufikia na kuvuka rekodi ya mfungaji bora wa muda wote Stars ambayo kwa sasa inashikiliwa na Mrisho Ngassa aliyepachika mabao 25.

Kwa sasa, Msuva amefumania nyavu mara 22 sawa na Mbwana Samatta na anaamini kwamba ana nafasi ya kumfikia Ngassa na kuandika rekodi mpya.

“ Namheshimu sana Mrisho Ngassa kwani yeye ni kaka yangu ni ‘role model’ (mfano wa kuigwa) kwangu na nampongeza kwa rekodi aliyoiweka kwani sio rahisi.”

SOMA NA HII  KUHUSU ILE ISHU YA FEI TOTO KUIPIGA CHINI YANGA...ALLY KAMWE LEO KAIBUKA NA HILI JIPYA...